Habari za Kitaifa

Familia ilimtafuta zaidi ya mwaka mmoja isijue alifia Shakahola

Na LUCY MKANYIKA  September 18th, 2024 1 min read

FAMILIA moja kutoka Mwatate, Kaunti ya Taita Taveta, inaomboleza baada ya kufahamishwa kwamba mwili wa jamaa yao aliyetoweka zaidi ya mwaka mmoja uliopita, ulitambuliwa miongoni mwa waliokufa Shakahola, Kaunti ya Kilifi.

Bi Jacinta Mzame, alisema walifahamishwa Jumamosi kwamba binti yake, Mary Mboli, alitambuliwa kupitia uchunguzi wa chembe za nasaba DNA.

Mary, mumewe na watoto wao watatu, walihamia Shakahola kutoka Likoni, Mombasa.

Mume wake amesemekana kuwa miongoni mwa washukiwa walio kizuizini, lakini hatima ya watoto hao bado haijulikani.

Kulingana na Bi Mzame, maelezo waliyopokea kufikia sasa ni kwamba mwili huo ulifukuliwa mnamo Mei 20, mwaka uliopita.

Familia imeanza mipango ya mazishi nyumbani kwao katika kijiji cha Mruru, lakini Bi Mzame anasema bado ana matumaini kuwa watoto waliopotea watapatikana.

‘Maumivu ya kumpoteza binti yangu yanachangiwa na sintofahamu ya kutojua hatima ya watoto wake, sijui wajukuu zangu wako wapi, dua zangu ni kwamba watoto wawe hai ili niwaone karibu yangu,’ alisema.

Aliongeza kuwa wanasubiri serikali kuwapa mwelekeo na kuwasaidia kujua waliko wajukuu zake.