• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Raia wa Argentina wagoma kulilia hali mbaya ya uchumi

Raia wa Argentina wagoma kulilia hali mbaya ya uchumi

Na AFP

SHUGHULI zilikwama Argentina kufuatia mgomo wa umma Jumanne uliosababishwa na matatizo ya kiuchumi yanayokabili taifa hilo.

Wakati huo huo, rais wa benki kuu nchini humo alijiuzulu huku serikali ikijitahidi kushauriana na Hazina ya Kimataifa ya Fedha (IMF) ili ipate mkopo wa dharura.

Huku Rais Mauricio Macri akiendeleza mashauriano ili kupokea ufadhili wa dola bilioni 50 kutoka kwa IMF, thamani ya sarafu ya nchi hiyo (peso) ilizidi kudorora huku habari zikicipuka kwamba Guido Sandleris alichukua mahali pa Luis Caputo kuwa msimamizi mpya wa benki kuu.

Raia karibu wote wa Argentina walifanya mgomo na baadhi wakaandamana kuonyesha ghadhabu yao kuhusu jinsi gharama ya maisha imekuwa ngumu kufuatia jinsi thamani ya pesa ilivyoshuka kwa karibu asilimia 50 dhidi ya dola mwaka huu.

Maduka mengi, mabenki na afisi za umma zilifungwa huku wahudumu wa uchukuzi wa umma na teksi wakilemaza shughuli za usafiri.

Baada ya maandamano ya Jumatatu yaliyoandaliwa na vyama vya wafanyakazi, waandamanaji wa upande wa upinzani waliungana nao Jumanne kukawa na makabiliano kati yao na maafisa wa usalama Buenos Aires mnamo Jumanne.

Barabara za katikati mwa jiji zilikuwa tulivu mno kwani hapakuwa na watu walioenda kazini.

Viwanja vya ndege pia havikuwa na watu wengi kutokana na kuwa usafiri wa ndege kuingia na kuondoka katika nchi hiyo ulifutiliwa mbali.

Mfumko wa kiuchumi unatarajiwa kupanda kwa asilimia 40 kufikia mwisho wa mwaka.

Hali ilianza kuwa mbaya Argentina kuanzia Aprili wakati thamani ya peso iliposhuka kwa kasi na serikali ikaomba mkopo wa dola bilioni 50 kutoka kwa IMF.

Hatua hii haikuleta afueni na Macri akatangaza Agosti kwamba ataomba mkopo uliotarajiwa kutolewa kwa awamu za miaka mitatu utolewe haraka mwaka huu.

Macri pia alitangaza mikakati mingine ya kupunguza matumizi ya fedha za umma ikiwemo kupunguza wizara za serikali kwa asilimia 50, na kurudisha ushuru wa nafaka zinazouzwa nje ya nchi.

Benki Kuu ilitoa taarifa kudai kuwa Caputo alijiuzulu “kwa sababu za kibinafsi” huku ikieleza matumaini yake kuwa “makubaliano mapya na IMF yatarudisha imani kwa hali ya kifedha na ubadilishanaji wa hisa za kigeni”.

Baadhi ya wachanganuzi walisema kulikuwa na uvumi Ijumaa iliyopita kwamba angejiuzulu kwa sababu ya “tofauti kati yake na IMF kuhusu sera za kifedha”.

Sandleris ni mwanauchumi ambaye aliwahi kufanya kazi katika Benki ya Dunia. Alikuwa naibu waziri wa fedha kabla kutangazwa kuwa rais wa benki kuu.

You can share this post!

Nyuki wavamia kijiji na kuua mwanamke na kondoo wake

TAHARIRI: Kampuni za kamari zifanyie spoti hisani

adminleo