• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
2019: Ukosefu wa usiri wa data mitandaoni utazidi kuwaumiza Wakenya mwaka huu

2019: Ukosefu wa usiri wa data mitandaoni utazidi kuwaumiza Wakenya mwaka huu

Na FAUSTINE NGILA

TEKNOLOJIA ya dijitali mwaka uliopita ilituwezesha kupata taarifa tunazotaka mitandaoni kwa urahisi zaidi ila bila kujali athari za kukubalia mitandao hiyo kutuchunguza.

Tulichohitaji kufanya ni kufungua tovuti kwenye intaneti na kujipakulia huduma kadha kama ununuzi wa bidhaa, upakuaji wa video na matini ya kusoma, na kurambaza mitandao ya kijamii bila vizuizi.

Hata hivyo, kupakua taarifa hizi humaanisha kukiuka kanuni kuhusu ukusanyaji wa data, matumizi yake na ulinzi wa taarifa zetu za siri.

Yamkini kila Mkenya hubonyeza maandishi ‘Ninakubali’ bila kusoma na kuelewa masharti ya tovuti nyingi kwenye intaneti, na hivyo kuziruhusu tovuti hizi kukusanya data kumhusu bila taarifa kutokana na uzembe wake wa kusoma.

Mwaka 2019 utazidi kuwa hivi, kwa kuwa kizazi cha dijitali hakipendi kabisa kudurusu maandishi ya masharti ya tovuti, programu za simu na mitandao ya kijamii kabla ya kupokea huduma zake.

Mwaka huu data zote za siri zitakuwa wazi kwa kuwa tunapopakua programu za simu, ujumbe wa onyo huja: ‘Je, ungependa kuiruhusu apu hii kukusanya data yako ya simu kuhusu orodha ya nambari za simu, picha, video, sauti, umri, jinsia, familia, ajira, nambari ya kitambulisho na historia ya intaneti?’

Wakenya wengi hubonyeza ‘Ndiyo’, na hapo ndipo tunazikandamiza sisi wenyewe haki zetu za usiri wa data.

Hii inamaanisha kuwa tumebadilisha imani na mtazamo wetu kuhusu usiri wa data na jinsi tunajithamini, na kukubali kuwa watumwa wa mitandao.

Na huu ndio mwaka utawasikia Wakenya wakilalamikia baada ya data za siri kuwahusu kutumika kwa shughuli nyingine, huku wakisahau wameiruhusu Google kukusanya na kuhifadhi taarifa kuhusu maeneo wanayozuru, wanakoishi na wanaotangamana nao.

Huku teknolojia ya dijitali ikizidi kuwa nguzo muhimu ya maisha ya Wakenya, tofauti ya taarifa za umma na data za kibinafsi itazidi kuwa finyu mwaka huu, na wataalamu wengi wanakubali mjadala kuhusu usiri na ulinzi wa data haupo tena.

Kulingana na Afisa Mkuu Mtendaji wa kampuni ya ulinzi wa data za mitandaoni GreyCastle Security, Bw Reg Harnish, dhana ya usiri wa data ni ndoto.

“Katika miaka ijayo, tutakuwa tukizungumza kuhusu usiri wa data jinsi tunavyotania simu za jamii,” anasema.

Anaelezea kuwa bado kuna manufaa ya ulimwengu usio na dhana ya sasa kuhusu usiri wa taarifa.

Tofauti na Amerika ambapo data hiyo hukusanywa na serikali kuwafaa wananchi wake, hapa nchini baadhi ya kampuni hutumia data kuhusu Wakenya kujinufaisha huku mianya ya wizi wa hela ikijitokeza.

“Uwepo wa data nyingi mikono mwa watu wachache ni hatari , lakini iwapo ulimwengu ambao utatumia data hiyo pamoja utaondoa hatari hiyo, hasa katika uvumbuzi wa teknolojia mpya zinazowafaa watu kijamii,” anasema.

Huu utakuwa mwaka ambao Wakenya watakubali kabisa kuuza usiri wao ili kupata starehe za mitandaoni, lakini hatimaye watachoka na kuamua kurudishiwa usiri wao.

Lakini suluhu ni nini? Badala ya kulaani jinsi habari zinapatika na kwa urahisi, Wakenya wanafaa kubuni mbinu za kuzuia ukusanyaji wa data muhimu kuwahusu.

Licha ya Sheria ya Habari na Mawasiliano kubuniwa Kenya, huenda isiwalinde Wakenya dhidi ya ukusanyaji wa data bila taarifa, kwa kuwa Wakenya wamezoea mtindo wa kuruhusu mitandao kupakua data zao.

Kutokuwa na habari

Tatizo ni kwamba hatujui aina ya data tunayosambaza kwa mitandao ya kijamii na idadi ya data hiyo, na kwamba hatuna mamlaka tena ya kurudisha data ambayo tayari tushasambaza.

Wakati sera za Facebook kuhusu ubinafsi wa data zinasema kampuni hiyo inaweza kukusanya data unayotengeneza au kuchapisha, inamaanisha kuwa posti zote ambazo umeunda lakini ukakosa kuchapisha pia zitakusanywa.

Kwa kuwa Wakenya wamekubali kuuza usiri wao ili wapate starehe za dijitali, kile ambacho ni hatari zaidi ni kukosa kuelewa madhara ya kufanya hivyo.

Ikumbukwe kuwa ukusanyaji wa data mitandaoni ni zaidi ya kutia neno siri kwa tovuti au kupakua apu, kwani runinga za dijitali na vituo vya Wi-Fi pia ziko mbioni kukusanya taarifa kukuhusu.

Mwishoni mwa mwaka huu, utapata kwamba taarifa zote kukuhusu zimekusanywa na kuhifadhiwa. Kando na machapisho ya mitandaoni, utashangaa kuwa mawazo na maamuzi yako pia yanajulikana.

Kukabili hili, tunafaa kuanza kujali kuhusu umuhimu wa kulinda data zetu za siri, na kusoma kwa makini masharti ya kuingia kwa baadhi ya tovuti, na kuwafunza watoto wetu kuhusu hatari iliyopo ya kuruhusu kampuni za dijitali kukusanya data zao.

Kwa mfano, tatizo la usiri wa data mwaka 2018 halikuwa udukuzi bali kampuni za teknolojia zenyewe, ambazo zilivuna milima ya data na kutumia mifumo ya hila kusambaza data hiyo kujinufaisha.

Sakata ya Facebook iliyohusisha kampuni ya Cambrige Analytica ilitokana na huduma ya Facebook kwa jina Facebook Graph API. Katika hali hiyo, Facebook iliundwa kukusanya data nyingi iwezavyo, kisha kuisambaza bila kujali kwa waundaji wa programu za simu.

Ikumbukwe kuwa hatari hii huleta athari za kisiasa, hasa baada ya kiongozi wa chama cha ODM kudai kuwa Cambrige Analytita ilichangia katika wizi wa kura katika uchaguzi mkuu wa 2017.

Iliripotiwa 2018 kuwa Facebook na Google zilishirikiana na benki na kununua data za kifedha kuhusu wateja wa benki hizo kisiri, hali ilizyozua maswali mazito kuhusu usiri wa data muhimu ya wateja.

Kampuni kama Yahoo na Facebook huwafungia nje watumizi ambao hawako tayari kuruhusu ukusanyaji wa data kuwahusu, hali ambayo inaibua hisia kuhusu iwapo 2019 tutahitaji sheria ya kimataifa kulinda data ya watumizi.

You can share this post!

Mama ashinda mashindano bila kumpa fahali wake bangi

Mbwembwe za Mwaka Mpya 2019

adminleo