Habari za Kitaifa

Gachagua, Sakaja wazidi kupakana tope hadharani

Na CHARLES WASONGA September 21st, 2024 2 min read

NAIBU RAIS Rigathi Gachagua amewaonya wale wanaopanga kuwasilisha hoja ya kumtimua afisini kwamba hatishiki huku akichochea mzozo kati yake na Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja.

Akiongea Ijumaa Septemba 20, 2024 alipowatembelea wafanyabiashara katika soko la mazao ya shambani la Marikiti, Nairobi, Bw Gachagua alisema yeye alichaguliwa na wananchi moja kwa moja na “siwezi kuondolewa afisini na watu wachache ambao wamenunuliwa.”

Serikali ya Kaunti ya Nairobi inataka kuwahamisha wafanyabiashara hao hadi soko jipya la kisasa liliko kando ya barabara ya Kangundo, eneo bunge la Embakasi Mashariki.

“Wale wanaopanga kuniondoa afisini nawaambia wathubutu. Ningependa kuonya dhidi ya kuniuzia woga ni Wakenya walionichagua walio na uwezo wa kunifuta kazi,” Bw Gachagua akaeleza.

Naibu Rais alisema kuwa hatatishwa kwa kusimama na Wakenya wenye mapato ya chini.

Bw Gachagua hakutaja watu ambao wanapanga njama ya kumwondoa afisini wala hatua ambayo wamepiga kufikia sasa. Lakini alisisitiza kuwa njama hizo hazitafaulu.

Juzi, wabunge wandani wa Naibu Rais walidai kuwa kuna njama ya kumwondoa afisini ili kusambaratisha kampeni zake za kujenga umoja wa kisiasa katika eneo la Mlima Kenya.

Walisema hayo siku chache baada ya angalau wabunge 50 kutangaza kuwa wanamtambua Waziri wa Usalama wa Ndani Kithure Kindiki kama msemaji wao na kiunganishwa kati yao na Rais William Ruto.

Bw Gachagua amekuwa akijinadi kama msemaji wa eneo la Mlima Kenya na mtetezi sugu wa masilahi ya wakati wa eneo hilo.

Mzozo na Sakaja

Jijini Nairobi, Gavana Johnson Sakaja alitangaza wiki jana kwamba serikali yake itawahamisha wafanyabiashara wa mboga na mazao mengi ya shambani kutoka soko la Marikiti ili kupunguza msongamano.

Lakini wafanyabiashara hao walifanya maandamano kupinga hatua hiyo wakisema wateja wao wako katikati mwa jiji.

Bw Gachagua pia alipinga hatua hiyo akisema uaumuzi kuihusu ilifikiwa bila kushirikishwa kwa maoni ya wafanyabiashara hao inavyohitajika kisheria.

Alimtaka Gavana Sakaja kukumbuka ahadi aliyowapa kuelekea uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022 kwamba angetekeleza sera za kuimarisha maisha yao.

Lakini Gavana huyo alijibu malalamishi ya akisema kuwa Bw Gachagua hafai kuwasiliana naye kupitia mitandao ya kijamii ilhali anayo nambari yake ya simu.

Ijumaa, Naibu Rais alirudia wito wake wa awali na kumtaka Gavana Sakaja kusitisha mpango wa kuwahamisha wafanyabiashara hao kutoka soko la Marikiti.