Dondoo

Kidosho avamiwa na nzi baada ya kupora mihela ya buda gesti

Na JANET KAVUNGA September 25th, 2024 1 min read

MSAMBWENI, KWALE

WAKAZI wa kijiji kimoja hapa walishuhudia tukio la kusikitisha, mwanadada mmoja alipovamiwa na jeshi la nzi saa chache baada ya kuonywa na buda mmoja kwamba angekiona cha mtema kuni kwa kupora pesa zake.

Haikubainika jinsi demu alivyopora pesa za mzee huyo lakini wakazi walishuku walikuwa wakiponda raha katika gesti mmoja.

“Watu walisikia buda akimuonya demu kuwa kama hangerudisha pesa zake, angejuta. Dakika chache baada ya kutoa onyo hilo, mzee aliondoka kwa gari lake na demu akaendelea na shughuli zake.”

“Hata hivyo, watu walishangaa alipovamiwa na nzi mwili mzima huku akionekana kutojali,” alisema mdokezi.

Demu alipoulizwa alichomfanyia buda huyo hakuweza kutoa sauti na watu wa familia wakalazimika kumtafuta buda ili kumuokoa binti yao.

Inasemekana walisaka nyumba ya demu wakapata bunda la pesa na kumpelekea mzee ndipo nzi wakaacha kumuandama.