Habari za Kitaifa

Jinsi Ruto amegusa mioyo ya wakazi wa Nyanza na kuwageuza waumini

Na GEORGE ODIWUOR June 3rd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

NYOTA ya kisiasa ya Rais William Ruto katika eneo la Nyanza inaendelea kung’aa zaidi kila kukicha huku imani ya wakazi kwa serikali yake ikiendelea kuimarika.

Kwa mfano, tofauti na mnamo Oktoba 2022 wakati alizuru Homa Bay kwa mara ya kwanza ambapo wakazi na viongozi walichelea kumpa makaribisho mazuri, wakati huu amekumbatiwa vilivyo kiasi cha kuahidi kumuunga mkono kwenye uchaguzi mkuu wa 2027.

Mapokezi baridi pia yalishuhudiwa Rais Ruto alipohudhuria hafla ya kusherehekea kuteuliwa kwa Katibu katika Wizara ya Usalama Raymond Omollo mnamo Julai 2023 katika kijiji cha Kanyipir, eneo bunge la Kasipul, Kaunti hiyo ya Homa Bay.

Wakazi wa Homa Bay waliofika uwanja wa Raila Odinga kwa Madaraka Dei wamshangilia Rais Ruto alipokuwa anaingia uwanjani. Picha|PCS

Shughuli hizo mbili zilionyesha wazi utofauti wa kisiasa kati ya utawala wa Rais Ruto na eneo la Nyanza ambalo ni ngome ya kisiasa ya aliyekuwa mshindani wake mkuu katika uchaguzi mkuu wa 2022, Raila Odinga.

Lakini hali ilibadilika baada ya maandamano ya Gen Z, mwaka jana Rais Ruto na Bw Odinga, ambaye ni kiongozi wa ODM walipoamua kuzika tofauti zao za kisiasa na kushirikiana kuleta utulivu nchini.

Dkt Ruto aliamua kuunda serikali jumuishi kwa kuwateua wandani watano wa Bw Odinga katika baraza lake la mawaziri.

Isitoshe, baada ya Rais Ruto na kiongozi huyo wa ODM kutia saini rasmi mkataba wa ushirikiano mnamo Machi 4, 2025, serikali ya kitaifa imeonekana ikipelekea maendeleo katika eneo la Nyanza.

Isitoshe, Rais Ruto amefanya angalau ziara nane katika kaunti ya Homa Bay tangu aliingia mamlakani akizindua miradi kadha ya maendeleo.

Kutokana na hilo, viongozi wa kaunti ya Homa Bay na eneo la Nyanza kwa ujumla sasa wanachangamkia utawala wa Rais Ruto wakiungana naye wakati wa ziara zake eneo hilo.

Kabla ya kuongoza sherehe za mwaka huu za Madaraka Dei katika uwanja wa michezo wa Raila Odinga, Dkt Ruto alifanya mkutano wake wa kwanza katika ikulu ndogo mpya ya Homa Bay ambapo waliwataka viongozi wa ukanda huo kuunga mkono serikali yake.

Umati mkubwa wa wakazi Homa Bay waliokosa viti wakaa chini kusikiliza hotuba ya Rais Ruto Juni Mosi wakati wa Madaraka Dei. Picha|PCS

Aidha, aliwataka wamsaidie kutekeleza ahadi alizotoa kwa raia wakati kampeni za kuelekea uchaguzi mkuu wa 2022.

Dkt Ruto alisema ujenzi wa Ikulu Ndogo Mjini Homa Bay ulikuwa ni hatua ya kimakusudi iliyolenga kuhakikisha kuwa wakazi wanahisi kushirikishwa katika serikali ya kitaifa.

Mkutano huo katika Ikulu hiyo ndogo pia ulishirikisha viongozi waliochaguliwa kutoka kaunti ya Homa Bay.

Miongoni mwa waliohudhuria ni Gavana Gladys Wanga, Seneta Moses Kajwang’, Mbunge Mwakilishi wa Kike Joyce Osogo na Mbunge wa Homa Bay Mjini Peter Kaluma.

Wengine walikuwa wabunge; Millie Odhiambo (Suba Kaskazini), Adipo Okuome (Karachuonyo), Caroline Omondi (Suba Kusini), Dkt Lilian Gogo (Rangwe) na Martin Owino (Ndhiwa) pamoja na madiwani, maafisa wa serikali ya kaunti miongoni mwa wengine.