Katibu asuta upinzani kwa kuwachochea Wakenya dhidi ya serikali
KATIBU Mkuu katika Idara ya ustawi wa mifugo Jonathan Mueke ametetea rekodi ya maendeleo ya serikali huku akisuta viongozi wa upinzani kwa kuchochea Wakenya dhidi ya utendakazi wa serikali ya Kenya Kwanza.
Akihutubia wakulima katika Kaunti ya Uasin Gishu kwenye ngome Rais William Ruto, Bw Mueke alionya Wakenya dhidi ya kunaswa na matamshi, siasa na propaganda zinazoenezwa na upinzani kote nchini.
Bw Mueke alisema serikali imejitolea kutekeleza miradi yote ya maendeleo iliyopangwa licha ya pingamizi kali kutoka kwa viongozi wa upinzani wanaolenga kuvuruga kila kitu ambacho utawala wa Kenya Kwanza unafanya.
“Tunafuraha kwamba Wakenya wameanza kufurahia matunda ya ajenda za serikali ya Kenya Kwanza kufikia sasa ambazo ni pamoja na kutekelezwa kwa huduma za afya kwa wote na mradi wa nyumba za bei nafuu kote nchini,” akasema Bw Mueke.
Bw Mueke alihakikishia wakulima kukumbatia mpango wa serikali wa kutoa chanjo ya ng’ombe milioni 22 na kondoo na mbuzi milioni 50 kote nchini.
Kiongozi huyo alisuta wansiasa ambao wamekuwa wakipinga mpango huo.
Aliwaambia wafugaji katika Bonde la Ufa kupuuza propaganda zinazoenezwa na wakosoaji wa serikali kuhusu usalama wa chanjo hiyo akibainisha kuwa ni salama na imeidhinshwa Taasisi ya Kuzalisha Chanjo za Mifugo ya Kenya (KEVEVAPI).
“Tangu serikali ilipoanzisha kampeni ya chanjo ya mifugo, nchi yetu imevutia masoko ya kimataifa ya bidhaa za mifugo baada ya kufikia viwango vya kimataifa,” alisema Mueke.