Maoni

MAONI: Raila daima anajua kusoma nyakati, kutembea na majira

Na PAUL NABISWA June 4th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

SIJUI aitwe Baba, waziri mkuu wa zamani ama kiongozi wa ODM. Napata taabu kidogo kujua jina linalomwafiki mwanasiasa nguli Raila Odinga.

Baadhi ya wandani wake wanamuita msaliti kwa kukubali kufanya kazi na Serikali Jumuishi ya Rais William Ruto.

Wengine wanadhania amepigania watu kwa muda mrefu anastahili kivuli cha pumziko. Wapo wanaohisi ni mtu wa kuyajali masilahi yake mwenyewe.

Wote wako sahihi.

Mgaala muue na haki yake umpe. Raila anajua kujenga virutubishi katika hoja zake kulingana na majira ili si kuwateka tu wanahabari bali pia hugusa nafsi za wananchi.

Katika sherehe za Madaraka, Homa Bay, Raila alimkumbusha Rais William Ruto kuwa anapongezwa kwa kuwaomba msamaha vijana wa Gen-Z ambao anadhania serikali na watu wa kizazi chake wamewafanyia madhila.

Kwa busara zake alisema msamaha hautoshi, familia za vijana waliouawa zinatakiwa kupewa ridhaa. Matamshi ya Raila yalikuwa na umuhimu mkubwa kwa Rais Ruto ikiwa angetaka kujisaidia.

Mwanzo, zaidi ya roho 60 zilizimwa na mitutu ya bunduki kwa hisani ya serikali ya Kenya Kwanza. Baadhi ya vijana hao walikuwa wameyabeba matumaini makubwa kwa familia zao.

Wazazi wakasalia na maswali mengi baada taa zao kuzimwa na nguvu za dola. Huyu ndiye Raila wa miaka ya kisogoni, aliyeonekana kuwa mtetezi wa haki za binadamu.

Raila amemwokoa Ruto kwa kujua ama kutojua. Kundi la Rigathi Gachagua lilikuwa limechukulia hoja ya msamaha kama mtaji wao mkuu katika siasa za 2027 na chambo cha kuwavua washiriki kutoka bahari ya Rais Ruto.

Naibu Kiongozi wa chama cha DCP Cleophas Malala alikuwa amemkumbusha Rais Ruto kuwa msamaha hautoshi, Rais anahitaji toba.

Akaongeza kuwa katika toba hiyo hiyo Ruto anatakiwa kutaja kila kosa na kuliombea msamaha. Rais ni mlokole na nadhani anafahamu utaratibu huo.

Wazo hili la Raila siyo bonzo, huenda alilifikiria kwa makini ikiwa si jambo lililomtoka sadfa.

Kwanza, amesema hoja hiyo wakati ni mwezi ambao mswada wa fedha wa 2025 ambao baadhi ya watu wamepiga kelele na unatakiwa kupitishwa bungeni.

Ni msimu kama huu mwaka uliopita vijana hao wa Gen – Z wenye damu changa walishangaza ulimwengu kwa kuvamia majengo ya Bunge baada ya mswada wa fedha wa 2024 kupitishwa.

Baadhi ya vijana wakati huu wanapinga mswada huo kwa dhati na inawezekana baadhi wanadhania kuwa serikali inataka kuwachezea shere kwa mara nyingine.

Rais angejikakamua na kuzifidia familia zilizoathirika mwaka uliopita pengine ingekosha nyoyo za vijana ambao vifua vyao vinawataka kuingia barabarani.

Paul Nabiswa ni mhariri, NTV