Habari

Gachagua: Ruto amesambaratisha elimu ya bure aliyoleta Kibaki, pesa amezipeleka kwa siasa

Na  LUCY MKANYIKA  June 8th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Naibu Rais Rigathi Gachagua amedai kuwa serikali ya Kenya Kwanza inatumia fedha za elimu kufadhili miradi ya kisiasa.

Akizungumza katika mkutano wa kisiasa mjini Voi, Kaunti ya Taita Taveta Juni 7, 2025, Bw Gachagua alisema kuwa wazazi watalazimika kulipa karo kwa watoto wao wa shule ya msingi na upili baada ya fedha za kufadhili elimu ya bure kufujwa.

Haya yanajiri baada kubainika kuwa serikali inadaiwa zaidi ya Sh64 bilioni ambazo zilipaswa kupelekwa kwa shule za umma.

Kutokana na hali hiyo, huenda wazazi wakalazimika kulipa karo baada ya zaidi ya miaka 20 ya elimu bila malipo.

Bw Gachagua alidai kuwa miradi ya kuwawezesha wananchi inayoongozwa na Naibu Rais Kithure Kindiki na washirika wa Kenya Kwanza inalenga kuwahadaa wananchi kwa fedha za serikali.

“Serikali imepanga bajeti ya Sh10 milioni kwa kila eneo bunge kwa miradi hii, lakini katika ngome ya Rais Ruto, kila eneo bunge limepangiwa Sh150 milioni. Fedha hizi zilipaswa kupelekwa kwa mfumo wa elimu ya bure,” alisema.

Aidha, alidai kuwa Rais Ruto anatumia miradi hiyo kuimarisha uungwaji mkono wake huku akipuuza maeneo mengine ya nchi.

Bw Gachagua pia alikosoa mkataba wa kisiasa kati ya Rais Ruto na Raila Odinga, akisema haukulenga kuleta umoja bali kutuliza maandamano ya vijana wa kizazi cha GenZ.

“Walisema wanaiunganisha nchi, lakini wanapotuona tukishirikiana na Kalonzo, wanatuita wakabila. Tunajua walikuja pamoja ili kuimarisha serikali yake na kuepuka hasira ya GenZ,” alisema Bw Gachagua.

Wakihutubia wakazi wa Voi, viongozi wa upinzani wakiongozwa na Bw Gachagua na kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka walitangaza kampeni kali za kisiasa za kumaliza utawala wa Rais Ruto katika uchaguzi wa 2027.

Kwa upande wake Bw Musyoka vilevile aliungana na Bw Gachagua kukosoa serikali kwa kutumia miradi ya kuwawezesha wanawake kisiasa.

“Wakenya wamechoshwa na uongo. Serikali ya Ruto imeshindwa, na sasa wanatumia miradi ya kuwawezesha wanawake kuwahadaa wananchi. Lakini Wakenya wameamua kuwa watawaondoa madarakani,” alisema.

Viongozi hao pia walitangaza Juni 25 kuwa siku ya kuwakumbuka waliouawa katika maandamano ya kupinga Mswada wa Fedha mwaka jana.

“Tutaiita Siku ya Mapinduzi ya GenZ. Vijana wataamua cha kufanya siku hiyo,” alisema Bw Kalonzo.

Seneta wa Kisii, Richard Onyonka, aliahidi kumfungulia mashtaka Rais Ruto baada ya kuondoka madarakani mnamo 2027 kwa madai ya ufisadi.

“Wanapora fedha za elimu, hospitali, hata ardhi na madini. Huu ni utawala wa muhula mmoja tu. Akiondoka madarakani, tutampeleka mahakamani,” alisema.