Wasomi wawili mashuhuri Ikulu walioshindwa kushuka chini kutatua shida za raia
KUINGIA Ikulu kwa William Ruto mwaka wa 2022 kama Rais wa tano wa Kenya kuliweka historia kwa nchi kuwa mikononi mwa mtu mwenye shahada ya Uzamifu (PhD) kwa mara ya kwanza.
Ingawa ni mara ya pili kwa nchi kuwa na Profesa (Kithure Kindiki) kama Naibu wa Rais, ni mara ya kwanza kwa nchi kuwa na viongozi wawili wenye PhD.
Profesa Kindiki anafuata nyayo za marehemu Profesa George Saitoti aliyehudumu chini ya rais wa pili, Daniel Moi.
Dkt Ruto aliposhinda, alichukua uongozi wa nchi ambayo ilianzishwa na msomaji wa mita za stima enzi za kikoloni kwa jina Jomo Kenyatta.
Bw Kenyatta alimwachia uongozi mwalimu Daniel Moi, mwaka 1978, ambaye naye alikabidhi kwa mwanauchumi Mwai Kibaki.
Bw Kibaki alimwachia Uhuru Kenyatta, mtaalamu wa sayansi ya siasa, ambaye Naibu wake alikuwa Bw Ruto, aliyekuwa na shahada ya kwanza ya Botania na Zoolojia na shahada ya uzamili ya Ekolojia ya Mimea.
Ilipofika mwaka wa 2018, alipata shahada ya Uzamifu (PhD) baada ya kukamilisha masomo ya Ekolojia ya Mimea katika Chuo Kikuu cha Nairobi (UoN).
Alihitimu baada ya miaka sita tangu Agosti 2012 alipoanza kusomea uzamifu.
Ruto alipotwaa urais, Naibu wake alikuwa Bw Rigathi Gachagua ambaye alikuwa na shahada ya kwanza na aliwahi kuhudumu kama Afisa wa Wilaya (leo hii Naibu Kamishna wa Kaunti).
Bw Gachagua katika mikutano mingi ya hadhara alimsifu bosi wake kama ‘msomi wa hali ya juu na mlezi mkubwa anayenitia moyo nikajisajili kusoma ili nipate hadhi kubwa pia.’
Ingawa taifa, hasa katika Mlima Kenya na Bonde la Ufa, lilipokuwa na matumaini Rais msomi angeponya matatizo ya nchi, wengi siku hizi wamefadhaika.
“Sio kwa sababu kuna jambo ambalo Dkt Ruto amefanya ambalo halijawahi kushuhudiwa nchini, bali kwa sababu alichukua mamlaka akiwa na hali ya kujiona bora zaidi ya Kenya na Wakenya wote,” asema mtaalamu wa siasa Bw Festus Wangwe.
Bw Wangwe asema Rais Ruto alikuwa na mawazo mazuri, hotuba nzuri, ahadi za kuvutia na maombi ambapo wafuasi wake walimwamini kama Masihi aliyekuwa akisubiriwa kwa muda mrefu.
Anaongeza kuwa elimu nzuri huja na kiburi, na hakuna kosa lolote kwa Dkt Ruto kujivunia akili yake, kupendekeza suluhisho za kitaaluma kwa changamoto za nchi, na kuamini angefanya Kenya ifikie hadhi ya fikra za PhD.
Hakufanikiwa kwani changamoto zilizomkumba hazikuheshimu elimu, bali zilihitaji suluhisho za moja kwa moja.
“Dkt Ruto alikuta madeni yaliyohitaji kulipwa, si kusomwa. Alikuta upinzani uliodai aliiba kura za 2022 na kilichohitajika ni kutumia maandamano kushinikiza kugawana mamlaka,” asema mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Kilimo na Teknolojia cha Jomo Kenyatta, Bw Charles Mwangi.
Bw Mwangi asema Rais Ruto aliahidi mengi, na wananchi walipoanza kutaka matokeo aliyokuwa ameahidi ndani ya siku 100 na mengine mara tu baada ya kula kiapo, shahada ya PhD haikuweza kuleta suluhisho.
Anaongeza: “Tumpatiehaki yake – kuwa Dkt Ruto si kazi rahisi. Hakuna ajabu aliyofanya katika uongozi wake, isipokuwa alitumia sayansi kupita kiasi katika kujaribu kutoa huduma.”
Bw Mwangi asema watangulizi wa Dkt Ruto waliondoka wakiwa na mzigo wa ufisadi, mauaji ya kiholela, ukabila, upendeleo, uchumi mbovu, masuala yale yale ambayo Dkt Ruto anapambana nayo kwa sasa.
Anasema changamoto ya Rais Ruto ni ya kisiasa na inahusiana na kushindwa kwake kutumia hekima ya kawaida ya ‘kushuka’ na kusikiliza wananchi wa kawaida.
“Alikua mkali sana katika kusisitiza kwamba angetuletea mbingu, hata wakati vitabu vya hesabu vya taifa vilikuwa wazi kuwa tunazama kiuchumi. Alitegemea mbinu za kisayansi zaidi kukusanya pesa kupitia ushuru kupita kiasi badala ya kupunguza mzigo wa raia,” alisema.
Mbunge wa Maragua Bi Mary wa Maua anamtetea Rais kwa kusema “Kwa kweli huyu ni rais atakayeponya nchi hii. Si daktari kwa kubahatisha tu.”
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Baraza la Watu Mashuhuri wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP), Bw Maina Kamanda, anasema ‘elimu nyingi imeaibishwa na Dkt Ruto.’
Bw Kamanda alisema kuwa ‘matokeo yanaonekana wazi kwa jinsi alivyojaribu kubadilisha historia yetu na mfumo wa kawaida wa kufanya mambo,kuanzia mabadiliko katika bima ya afya, ufadhili wa elimu ya juu, biashara za mashaka katika ushirikiano wa sekta ya kibinafsi na ya umma (PPP), hadi kuvuruga sera yetu ya kutounga upande wowote katika masuala ya kigeni.’
Bw Kamanda alisema kuwa ni roho ya kisayansi ndani ya Dkt Ruto iliyomfanya kuvuruga ngome zake 2022 na kuamua kumtimua Gachagua madarakani.
Profesa Kindiki alipata Shahada ya Sheria (LLB) kutoka Chuo Kikuu cha Moi mwaka wa 1988 kabla ya kuendelea kupata Shahada ya Uzamili (LLM) katika Sheria za Haki za Kibinadamu za Kimataifa na Demokrasia kutoka Chuo Kikuu cha Pretoria, Afrika Kusini mwaka 2000.
Pia alihudhuria mafunzo ya Diploma ya Uzamili katika Masomo ya Sheria katika Chuo cha Sheria cha Kenya mwaka 2001 baada ya kumaliza shahada yake ya kwanza. Mnamo 2002, alihitimu na Shahada ya Uzamifu (PhD) katika Sheria za Kimataifa kutoka Chuo Kikuu cha Pretoria.
Seneta wa Meru, Bw Kathuri Murungi anaamini kuwa Profesa Kindiki amekuwa msaada mkubwa wa kiakili kwa rais.
“Prof Kindiki amemsaidia rais kuleta uthabiti katika urais na katika nchi. Ameondoa ufisadi katika idara ya uhamiaji, ameweka msingi wa kushinda magaidi na majambazi, na pia kusaidia urais kuleta mabadiliko mashinani kupitia miradi ya kuwawezesha wananchi,” alisema.