Habari za Kitaifa

Maandamano ya kulaani mauaji ya Ojwang yateka jiji ujumbe ukitolewa, ‘hiki ni kionjo’

Na WAANDISHI WETU June 13th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WAKENYA wanaendelea kushinikiza haki kutendeka kufuatia kifo cha mwalimu na mwanablogu Albert Ojwang akiwa mikononi mwa maafisa wa polisi.

Jana, mamia ya vijana waliandamana katika barabara za jiji kuu la Nairobi wakimtaka Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat ajiuzulu kufuatia madai kwamba alihusika na mauaji ya Albert Ojwang.

Waandamanaji walizunguka katika barabara muhimu katikati ya jiji huku polisi wakiwarushia vitoa machozi kuwazuia wasifike makao ya bunge ambako Waziri wa Fedha John Mbadi alikuwa akisoma bajeti ya mwaka wa kifedha wa 2025/2026.

Baadhi walisikika wakiimba bila haki, hakuna bajeti, Pia walifunga barabara kuu kama Harambee Avenue, jambo lililotafsiriwa kama jaribio la kupenya ulinzi mkali uliowekwa kuzunguka Bunge.

Magari mawili yalichomwa karibu na Kenya Cinema dakika chache kabla ya Bw Mbadi kuanza kusoma bajeti.

Polisi walitumia vitoa machozi na mbinu nyingine za kudhibiti umati kuwatawanya waandamanaji.

Waandamanaji katika barbara ya Harambee Avenue Juni 12, 2025. Walilaani mauaji ya Albert Ojwang wakitaka Naibu Mkuu wa Polisi Albert Lagat ajiuzulu. Picha|Wilfred Nyangaresi

Baadhi ya waandamanaji walionekana wamevalia mavazi ya rangi za bendera ya Kenya, huku wakiimba kwa sauti ya pamoja wakishinikiza kujiuzulu kwa Naibu Inspekta Jenerali kufuatia kifo cha mwanablogu, Albert Ojwang, aliyefariki akiwa mikononi mwa polisi.

Ojwang alikamatwa nyumbani kwake Homa Bay na kusafirishwa hadi Nairobi ambako alifariki kwa kupigwa ilivyoonyesha ripoti ya upasuaji wa maiti.

Waliotumia barabara ya Thika waliripoti ukaguzi mkali ambapo maafisa walikuwa wakikagua magari kwa makini ili kupunguza idadi ya magari yanayoingia CBD.

Baadhi ya biashara zilifungwa kwa hofu ya uporaji.

Licha ya ulinzi mkali, waandamanaji walionekana kuwa thabiti wakiendelea kuandamana kupitia barabara mbalimbali katikati kwa jiji wakitaka haki kwa Ojwang.

Haya yalijiri wakati wakuu wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS), wakiongozwa na Inspekta Jenerali Douglas Kanja na Mkuu wa DCI Mohamed Amin, walipokuwa mbele ya Kamati ya Bunge ya Usimamizi na Usalama wa Ndani kujibu maswali kuhusu kifo cha Ojwang.

Mwenyekiti wa Mamlaka Huru ya Kusimamia Utendakazi wa polisi (IPOA) Isaak Hassan alifika mbele ya kamati hiyo inayoongozwa na mbunge wa Narok Magharibi Gabriel Tongoyo.

Bw Tongoyo aliomba Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetangula kuruhusu kamati yake kuwasilisha ripoti yake Jumanne wiki ijayo.

Hata hivyo, alifichua kuwa IPOA ilieleza kamati kwamba tayari imetambua maafisa watatu wa polisi waliohusika na mauji ya Ojwang na ambao inapendekeza wakamatwe wakati wowote.

Hata hivyo, hakufichua majina au cheo cha maafisa hao ambao Bw Isaak alitaja katika kikao cha faraghani na kamati hiyo.

Kwenye mitandao ya kijamii, Wakenya waliendelea kuunga familia ya Ojwang kwa kuchanga fedha wakati huu mgumu na hata baada ya mazishi.

Kifo chake kimeunganisha taifa, wengi wakidai haki itendeke kwa familia hiyo.

Kinachozidi kuwaunganisha Wakenya ni juhudi za mchekeshaji maarufu Erick Omondi, kupitia mpango uitwao Sisi kwa Sisi — kampeni ya mtandaoni aliyozindua kusaidia familia zilizo katika matatizo ya kifedha na kisaikolojia.

Walter Opiyo wa Bunge La Wananchi na pamoja na wanachama Okano Nyasanga na Evance Oloo, walidai kuwa matokeo ya uchunguzi wa mwili wa marehemu yameonyesha wazi kuwa aliteswa hadi kufa.

“Imebainika kuwa Albert aliteswa hadi kufa na polisi wana kesi ya kujibu. Aliyetoa amri ya kumpiga anapaswa kutimuliwa kutoka kwa kikosi cha polisi,” alisema Opiyo.

Alimlaumu Lagat, aliyekuwa amelalamikia kwamba Ojwang alimchafulia jina kwa chapisho mtandaoni.

“Kujiuzulu kwa Lagat kutaruhusu uchunguzi huru na wa haki kufanyika ili familia ya Albert ipate haki,” alisema.