Ruto alitumia siku 156 kati ya 1000 madarakani akiwa nje ya nchi
RAIS William Ruto alitumia siku 156 za siku zake 1000 madarakani, akiwa nje ya nchi huku ziara 84 za kimataifa alizofanya kufikia sasa zikikosolewa.
Hata hivyo, amekuwa akitetea mara kwa mara safari zake akisema ni muhimu kwa kuvutia uwekezaji wa kigeni na kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia.Kati ya Septemba 2022 na Desemba 2024, Afisi ya Rais ilitumia Sh415.31 milioni kwa safari za nje pekee.
Hii ni sawa na kiwango cha wastani cha Sh450,000 kwa siku au Sh4.9 milioni kwa kila safari.Katika mwaka wa kwanza wa urais wake, rekodi kutoka kwa Mdhibiti wa Bajeti (CoB), zinaonyesha kuwa katika mwaka wa fedha wa 2022/2023 Afisi ya Rais ilitumia Sh361.77 kwa safari za nje, ikiwa ni kiwango cha juu zaidi kilichowahi kutumiwa na rais yeyote wa Kenya kwa mwaka mmoja.
Alikuwa amefanya safari 26 katika kipindi hicho.Safari za ndani za Afisi ya Rais pia zilikuwa juu zaidi kuliko ilivyokuwa awali, zikifikia Sh1 bilioni katika mwaka huo wa kifedha.
Hali hii ilisababisha hasira na ukosoaji kutoka kwa Wakenya wengi, wakishindwa kuelewa manufaa ya safari za Rais Ruto duniani kote.Katika mwaka wa 2023, Rais alifanya safari nyingi zaidi kuliko mwaka mwingine wowote, akiwa na safari 35.
Alienda Ulaya mara 10, Afrika mara 19, Asia mara mbili, alirudi Amerika kwa kwa mkutano wa Umoja wa Mataifa (UNGA) na alitembelea Mashariki ya Kati mara tatu.
Katika mwaka wa kifedha wa 2023/2024, Afisi ya Rais ilitumia tena Sh36.65 milioni kwa safari za nje, zikipungua pakubwa kutoka Sh361.77 milioni mwaka uliotangulia.
Hata hivyo, alifanya safari 38 katika mwaka huo wa kifedha, ikiwa ni idadi kubwa zaidi kwa rais yeyote katika mwaka mmoja.
Katika mwaka wa kifedha wa 2023/2024, safari za nje za serikali kuu ziliongezeka kwa karibu Sh3bilioni kutoka Sh6.3 bilioni katika mwaka wa kifedha wa 2022/2023 hadi Sh9.1 bilioni katika mwaka wa kifedha wa 2023/2024.
Safari bara UlayaMnamo mwaka wa 2023, Rais Ruto alifanya safari 10 barani Ulaya, ikiwa ni pamoja na ziara Ufaransa, Ubelgiji, Uswisi, Uholanzi na Ujerumani akihudhuria mikutano mbalimbali.
Alizuru mataifa ya Afrika mara 19, Asia mara mbili -China na India kwa ziara rasmi.Alirudi New York kwa mkutano wa Umoja wa Mataifa, UNGA mnamo Septemba na alitembelea Mashariki ya Kati mara tatu akifanya ziara mbili nchini Saudi Arabia kwa Mkutano wa Saudi-Afrika na mara moja Falme za Kiarabu (UAE) kwa Mkutano wa COP28.
Kabla ya maandamano makubwa dhidi ya mswada wa Fedha, mnamo Juni 18, 2024, Rais alikuwa amefanya safari 20 katika nchi 17, ikiwa ni pamoja na ziara za Kiserikali Japan mnamo Februari, Ghana mnamo Aprili na Amerika mnamo Mei.
Pia alihudhuria mikutano Korea, Italia-Afrika na UAE na akarudi Italia kwa mkutano wa G7 mnamo Juni 14, 2024.Hata hivyo, aliepuka safari za nje baada ya maandamano dhidi ya mswada wa Fedha.
Hakusafiri nje mnamo Julai na alifanya safari ya siku moja Rwanda mnamo Agosti kuhudhuria kuapishwa kwa Rais Paul Kagame.
Aliendelea na safari mnamo Septemba alipohudhuria Mkutano wa Ushirikiano wa China-Afrika nchini China na baadaye alihudhuria Tamasha la Mwaka la Wananchi mjini Berlin, Ujerumani katika mwezi huo huo.Kwa jumla, alifanya safari 29 mnamo 2024, ikiwa ni pamoja na nne za Ulaya, 18 za Afrika, tatu za Asia, mbili Amerika, moja ya Haiti na moja ya Mashariki ya Kati.
Kati ya Julai na Desemba 2024, Afisi ya Rais ilitumia Sh16.89 milioni kwa safari za nje.
Mwaka huu wa 2025, Rais amefanya safari 11 nje ya nchi kwenda Uganda, Ethiopia, Namibia, Ghana, mara mbili Tanzania, Angola na Ziara ya Kiserikali nchini Misri.
Nje ya Afrika, amefanya ziara ya Kiserikali kwenda China mnamo Aprili na pia alitembelea UAE na Vatican kwa mazishi ya Papa Francis.
Katika kipindi cha siku 1,000 za awali za urais wake, Rais Ruto alifanya safari za nje 84, akizidi idadi ya safari 53 alizofanya Rais mstaafu Uhuru Kenyatta katika kipindi kama hicho.
Hata hivyo, Rais Kenyatta alitumia jumla ya Sh502.5 milioni kwa safari hizo, ikiwa ni zaidi ya Sh415.31 milioni alizotumia Rais Ruto katika kipindi hicho hicho.
Kwa ujumla, Rais Kenyatta alifanya safari 158 za nje na kutumia jumla ya Sh1.6 bilioni kati ya Julai 2013 na Juni 2022, kulingana na ripoti za Mdhibiti wa Bajeti.
Kwa upande mwingine, Rais Ruto tayari ameweka rekodi ya kufanya safari nyingi zaidi kuliko Rais Kenyatta katika kipindi cha miaka miwili, na anaweza kufikia hadi safari 180 ifikapo mwisho wa muhula wake wa miaka mitano, ikiwa ataendelea na angalau safari tatu kwa mwezi.