Makala

Kubweka bila kung’ata: Ufisadi wazidi licha ya Rais kuahidi kuuzima

Na COLLINS OMULO June 13th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

KATIKA kampeni za uchaguzi wa 2022, Rais William Ruto aliahidi kwamba, endapo Wakenya wangemchagua kumrithi Rais Uhuru Kenyatta, serikali yake isingekubali ufisadi.

Aliweka wazi kuwa kila senti ingehesabiwa na hakuna fedha zitakazopotea.Alisema, “Nikipata nafasi ya kuongoza serikali, hakutakuwa na ufisadi kwa sababu hakutakuwa na fedha za kuiba; kila senti itatumika. Hakutakuwa na senti yoyote itakayozunguka ili mtu kuiba. Serikali itafanya kazi kama saa,” alisema Dkt Ruto Januari 2020.

Hata hivyo, Rais amekumbwa na shinikizo kwa kushindwa kuchukua hatua madhubuti dhidi ya watumishi wa umma wanaoshukiwa kuhusika na ufisadi, huku baadhi yao wakijivunia kwa kushindwa kwake kuweka msimamo madhubuti katika vita dhidi ya ufisadi.

Ripoti ya Tume ya Huduma za Umma (PSC) ya mwaka wa kifedha wa kwanza wa utawala wake, inaonyesha kuwa serikali ilipoteza Sh650 milioni kupitia mikataba ya ufisadi katika kipindi hicho.

Katika mwaka huo, kesi 109 za ufisadi ziliripotiwa, lakini Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) iliwafikisha mahakamani watumishi wa umma 34 pekee, na ni wanne tu waliohukumiwa.Kenya ilishuka nafasi tatu kutoka nafasi ya 123 hadi 126 kati ya nchi 180 katika orodha ya nchi zinazoongoza kwa ufisadi duniani kwa mujibu wa shirika la Transparency International.

Lakini je, kushindwa kwa Rais kuweka msimamo madhubuti dhidi ya ufisadi aliposhika madaraka kulichangia ongezeko la watumishi wa umma wanaoshukiwa kwa ufisadi?

Katika hotuba yake kwa Bunge Septemba 2023, Rais Ruto alikosolewa na upinzani kuhusu kujitolea kwake na azma yake dhaifu ya kupambana na ufisadi. Mbunge Maalum John Mbadi, ambaye sasa ni Waziri wa Fedha, alimshutumu Rais kwa kushindwa kuelezea mpango wa serikali yake wa kupambana na ufisadi nchini.

“Sielewi kwa nini Rais anapata ugumu kuita ufisadi kuwa ufisadi. Atakata kona na kutumia lugha inayokaribia ufisadi, lakini hakusema moja kwa moja,” alisema Bw Mbadi.

Licha ya kutishia mara kwa mara kuchukua hatua dhidi ya maafisa wa umma wanaohusika na ufisadi, na kujitolea kuongoza vita dhidi ya wizi wa mali ya umma katika ngazi zote za serikali, hajachukua hatua kubwa kufanikisha vita hivyo

.Mwaka mmoja baada ya kuchukua madaraka, kashfa kadhaa zilitikisa serikali ya Kenya Kwanza, ikiwa ni pamoja na zabuni ya vyandarua vya mbu ya Mamlaka ya Usambazaji Dawa Kenya (Kemsa) ambapo mamilioni ya fedha yaliporwa na maafisa wa serikali wasio waaminifu.

Kashfa nyingine ni ile ya sukari ya sumu ambapo maafisa wakuu wa serikali walishukiwa kwa njama ya kuiba sukari ya thamani ya Sh20 milioni.Kashfa nyingine ni ile ya mbolea ya ruzuku ya Sh10 bilioni, na ile ya mafuta ya kupika ya Sh6 bilioni.

Kashfa hizi zilijitokeza licha ya Rais kuahidi kwa nguvu akiwa Kaunti ya Murang’a, kuongoza vita dhidi ya ufisadi, akisema kuwa hakuna watakaosamehewa katika utawala wake.

“Nitajitolea binafsi kwa uwajibikaji wa rasilmali za nchi hii. Hakuna atakayekubaliwa kuiba rasilimali ya umma. Jaribu na utakutana nami,’ alisema Rais Ruto wakati wa mazishi ya David Waweru Ng’ethe katika Kaunti ya Murang’a Mei 2023.

“Nimeambia kila mtu, marafiki zangu na wasio marafiki zangu, kwamba kuharibu rasilimali za umma hakutakubalika. Nitakuwa nikizungumza kidogo kuhusu hili, lakini vitendo vitatangaza nia yangu kwa sauti kubwa.” Licha ya onyo hilo, mapepo ya ufisadi yameendelea kutawala, huku maafisa wa serikali katika utawala wake wakikumbwa na kashfa moja baada ya nyingine.

Akiongoza Madaraka Dei ya 61 huko Kakamega mwaka jana, Dkt Ruto alisema hatavumilia mtu yeyote atakayehujumu rasilimali zinazostahili kwa umma.

“Tutahakikisha tunashughulikia changamoto ya ufisadi, matumizi mabaya ya fedha na matumizi yasiyo ya lazima ya rasilimali za umma,” alisema Rais. ‘Naahidi kutowaangusha; utawala huu hautawaangusha.

“Matamshi haya yalijibu wasiwasi mkubwa miongoni mwa Wakenya kuhusu kuongezeka kwa kesi za ufisadi na matumizi mabaya ya rasilmali na maafisa wa umma.Lakini hakuna kinachoonyesha kuwa matamshi ya Rais yalikuwa ni maneno tu kama ushuhuda wa aliyekuwa Mwanasheria Mkuu na Waziri wa Huduma za Umma, Justin Muturi, aliyeanika siri kuhusu jinsi alivyoshinikizwa kuidhinisha mikataba ya mabilioni ya shilingi akiwa madarakani.

Alidai kuwa Rais Ruto alimsukuma kuidhinisha mkataba wa Sh129 bilioni kufadhili mradi wa upandaji miti, akiepuka wizara ya fedha kinyume na taratibu za kisheria.

“Niliposikia Ruto akisema havumilii ufisadi katika serikali yake, nilijiuliza anamaanisha nini,'”aliongeza.Rais William Ruto amekosoa mashirika ya uchunguzi, ikiwa ni pamoja na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP) na Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC), kwa kushindwa kushughulikia kesi za ufisadi katika mahakama.

Katika hotuba yake ya hali ya taifa aliyoitoa Bungeni, Rais alielezea wasiwasi wake kuhusu kushindwa kwa mashirika haya katika kuchunguza na kufikisha wahusika wa ufisadi mbele ya sheria. Rais alielezea kuwa hatua za kupambana na ufisadi zitafanikiwa tu ikiwa mashirika haya yatajitokeza na kutimiza matarajio ya wananchi kuhusu ufanisi na uwazi.

Aidha, Rais alikosoa Mahakama kwa kuchelewesha kesi za ufisadi na kudai kuwa hakuna sababu ya kesi hizi kudumu kwa miaka mingi wakati Mahakama zina uwezo wa kutatua kesi za uchaguzi ndani ya miezi sita.