Habari

Mashambulizi yachacha Israel ikionya itaangamiza Iran

Na REUTERS June 14th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

IRAN na Israeli zilishambuliana kwa makombora na mashambulizi ya angani siku ya Jumamosi, siku moja baada ya Israeli kuzindua mashambulizi makubwa dhidi ya adui wake wa muda mrefu, kwa lengo la kuzuia Iran kujenga silaha ya nyuklia.

Jijini Tehran, runinga ya taifa ya Iran iliripoti kuwa takribani watu 60, wakiwemo watoto 20, waliuawa katika shambulizi la kombora lililolenga jengo la makazi, huku mashambulizi mengine yakiripotiwa kote nchini humo. Israeli ilisema ililenga zaidi ya maeneo 150.

Nchini Israeli, milio ya ving’ora vya tahadhari iliwafanya wakazi kukimbilia hifadhi za dharura, huku makombora yakichana angani na makombora ya kujihami yakijibu. Takribani watu watatu waliuawa. Afisa mmoja wa Israeli alisema Iran ilirusha makombora 200 ya masafa marefu kwa awamu nne.

Rais wa Amerika Donald Trump aliunga mkono mashambulizi ya Israeli na kutoa onyo kwamba hali inaweza kuwa mbaya zaidi iwapo Iran haitakubali kupunguza shughuli zake za nyuklia kwa kiwango kikubwa, kama Amerika ilivyoitaka katika mazungumzo yaliyopaswa kuanza tena Jumapili.

Hata hivyo, Israeli ilisema operesheni yake itaendelea kwa wiki kadhaa, na ikaomba wananchi wa Iran waasi watawala wao wa Kiislamu. Hofu imeongezeka kuwa vita vya kikanda vinaweza kuzuka, vikihusisha mataifa ya nje na kuathiri uchumi na masoko ya fedha duniani.

Maafisa wawili wa Amerika walisema nchi hiyo ilisaidia kuzuia baadhi ya makombora ya Iran yaliyoelekezwa Israeli.

Hata hivyo, baadhi ya makombora ya Iran yaligonga maeneo ya makazi ya watu nchini Israeli. Waziri wa Ulinzi wa Israeli, Israel Katz alisema uongozi wa Iran “umevuka mpaka hatari. ”

“Ikiwa Ayatollah Ali Khamenei ataendelea kurusha makombora dhidi ya raia wa Israeli, basi Tehran itachomeka,” alisema katika taarifa.

Iran ilikuwa imeapa kulipiza kisasi mashambulizi ya Ijumaa, ambayo yaliwaua makamanda wa kijeshi na wanasayansi wa nyuklia, na kuharibu vituo muhimu vya nyuklia na kijeshi.

Iran pia ilitoa onyo kwa washirika wa Israeli, ikisema vituo vyao vya kijeshi katika eneo hilo vitashambuliwa iwapo vitashiriki kudungua makombora ya Iran, kwa mujibu wa runinga ya taifa ya Iran.

Huko West Bank, kundi la Houthi kutoka Yemen linaloungwa mkono na Iran lilirusha makombora usiku wa Ijumaa, ambapo kombora moja lilionekana kupotea njia na kuwajeruhi Wapalestina watano, wakiwemo watoto watatu, kwa mujibu wa Shirika la Msalaba Mwekundu la Palestina.

Hata hivyo, miaka miwili ya vita Gaza na mapigano Lebanon yamewaathiri washirika wa karibu wa Iran — Hamas na Hezbollah — na hivyo kupunguza uwezo wa Iran kujibu mashambulizi kikamilifu.