Pigo kwa Ruto chama cha Kiraitu, Mbus, kikihamia kwa Gachagua
CHAMA cha Devolution Empowerment Party (DEP) cha aliyekuwa gavana wa Meru Kiraitu Murungi kimejiunga rasmi na mrengo wa kisiasa wa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kwa kile kinachosema ni pambano la kuikomboa nchi kutoka kwa utawala mbaya.
Wakati wa Mkutano Mkuu wa Kitaifa wa wajumbe wa chama uliofanyika mjini Embu Jumatatu, DEP, maarufu kama “Bus”, ilitangaza nia yake ya kushirikiana na upinzani kuhakikisha kuwa Rais William Ruto atahudumu kwa muhula mmoja pekee.
Wakiongozwa na mwenyekiti wa kitaifa, Bw Lenny Kivuti, wajumbe hao walisema kuwa serikali ya Rais Ruto imepoteza umaarufu na hawataki kuhusishwa nayo.
“Tumeamua kuwasikiliza wananchi mashinani na kusikiliza matakwa yao ya pamoja,” alisema Bw Kivuti.
Wajumbe hao waliahidi kujiunga na upande ambao unaungwa mkono na Wakenya wengi.
“Tumeamua kuunganisha DEP na vuguvugu maarufu la ndugu zetu, lakini bila kuungana rasmi na chama chochote. Hatutaki kufanya makosa, tunataka kwenda kule Wakenya wako. Tutafanya kazi na Gachagua, Kalonzo Musyoka, Eugene Wamalwa, Uhuru Kenyatta, Justin Muturi, George Natembeya na Martha Karua ili kuikomboa nchi kutoka minyororo ya ukandamizaji,” alieleza Bw Kivuti.
Wajumbe hao walisema kuwa Rais Ruto amewavunja moyo Wakenya na anapaswa kujiandaa kuondoka madarakani.
“Tumekubaliana kuwa serikali hii itakuwa tu ya muhula mmoja,” alisema Bw Kivuti.
Wajumbe hao walikosoa serikali kwa mauaji ya kiholela, gharama ya juu ya maisha, na kushindwa kutekeleza majukumu yake.
“Wakenya, hasa wale wa Embu, wameumia chini ya utawala huu na tutaungana na upinzani kuiondoa serikali hii kupitia kura,” alisema Bw Kivuti.Aliahidi kuwakaribisha viongozi wa upinzani katika Kaunti ya Embu kuendesha kampeni dhidi ya serikali ya Kenya Kwanza ambayo alisema imepoteza mwelekeo.
DEP inalenga kuwa na wagombeaji katika nyadhifa zote katika kaunti ya Embu katika uchaguzi wa 2027.
Mkakati huo pia utatekelezwa katika kaunti nyingine kote nchini.
DEP pia italenga kushirikisha kizazi cha Gen Z na kuwajumuisha katika shughuli zote za chama na miradi ya maendeleo.
Zaidi ya hayo, DEP itatetea haki za wanawake, watu wenye ulemavu na makundi yaliyotengwa katika jamii ili kuwasaidia kuishi maisha yenye thamani, tija na heshima.
Wakati wa mkutano huo, wajumbe wa DEP walikubaliana kumuunga mkono na kumpigia debe Newton Kariuki ambaye ametangaza nia ya kugombea kiti cha ubunge cha Mbeere Kaskazini.
Bw Kariuki, ambaye kwa sasa ni mwakilishi wadi wa Muminji, atagombea kwa tiketi ya chama cha Democratic Party (DP).
Kariuki atagombea kwa tiketi ya DP ambacho ni chama rafiki kwetu na tutamuunga mkono,” alisema Bw Kivuti.
Waziri wa zamani wa Utumishi wa Umma, Bw Muturi kwa sasa ndiye Kiongozi wa DEP, Kiraitu Murungi, hakuhudhuria mkutano huo.