Akili MaliMakala

Teknolojia ya chupa za plastiki kuendeleza kilimo

Na SAMMY WAWERU June 18th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

JE, baada ya kushabikia kinywaji kilichositiriwa na chupa ya plastiki, huwa unafanya nini na chupa hiyo?

Wengi huweka chupa za plastiki kwenye mapipa au kwenye majaa. Cha kushangaza zaidi, wapo wanaozitupa kiholela barabrani. Plastiki huchukua miongo mingi kuoza, na utupaji wake usiofaa umechangia kwa kiasi kikubwa athari za mabadiliko ya tabianchi.

Kwa Patricia Makele, mwanafunzi wa chuo kikuu anayesomea Digrii ya Masuala ya Sayansi ya Mazingira, chupa hizo za plastiki ni raslimali ya thamani.

Patricia huzigeuza kuwa mfumo wa kunyunyizia mimea maji kwa njia ya matone, teknolojia faafu maeneo kame. Uundaji wake unajumuisha chupa ya plastiki, kipande cha mbao, na mrija wa soda.

Kijana mshirika wa Makele Youth Group akielezea kuhusu teknolojia ya plasiki kuendeleza kilimo. Picha|Sammy Waweru

“Shimo dogo hutobolewa chini ya chupa, mrija unawekwa kwa ajili ya kudondosha maji polepole, na sehemu za kuvuja hufungwa kwa guluu,” anaelezea.

Mbao za kutengeneza huzitoa kwa karakana za seremala, na chupa zikiwa zile zilizotupwa, hivyo basi ni malighafi au raslimali zinazopatikana humu nchini. Baada ya chupa kushughulikiwa, hufungwa kwenye mbao kwa mkanda wa plastiki.

Wazo hilo, Patricia anadokeza kwamba lilizaliwa alipokuwa kidato cha pili katika shule ya Precious Blood Riruta mwaka 2018. “Nilitumia kipaji changu cha sanaa kutengeneza maua kutoka kwa malighafi yanayochukuliwa kuwa taka ili kufariji mwanafunzi aliyekumbwa na changamoto.

Maua yanatumika kama ishara ya kufariji mtu, na mwalimu mkuu  alipogundua kipaji changu aliniunga mkono na kunipiga jeki,” akaambia Akilimali kwenye mahojiano ya kipekee.

Mfumo wa teknolojia ya chupa za vinywaji haswa soda, ni faafu hasa maeneo ya mijini. Picha|Sammy Waweru

Mengine yamekuwa historia, na hivyo ndivyo alivyoishia kuzindua Makele Youth Drive, mradi anaotumia kuhamasisha upanzi wa miti na mimea kwenye shule mbalimbali Nairobi, Machakos, na Kajiado.

Aidha, shirika hilo la vijana linahamasisha uhifadhi wa mazingira kupitia sanaa – teknolojia ya chupa za plastiki kuendeleza kilimo mijini na maeneo kame.

“Uhifadhi wa mazingira, kampeni yake inapaswa kuanzia kwa watoto – shuleni ili kukuza kizazi kijacho cha wanamazingira na wakulima,” Patricia anaamini.

Ubunifu wake, umetambulika na kuidhinishwa na Mamlaka ya Kitaifa ya Usimamizi wa Mazingira (NEMA). Patricia anasema mfumo huo huachilia tone moja la maji kila dakika na unaweza kuhudumia mmea wiki nzima.

Chupa inaunganishwa na kipande cha mbao, na kutobolewa shimo kudondoa maji. Picha|Sammy Waweru

Kufikia sasa, anahudumu na zaidi ya shule 15 katika kaunti lengwa, kwa ushirikiano na kundi lake la vijana wakisaidia kufanikisha mpango wa Kuungana, Kufanya, Kusaidia, Kenya, ndio 4-K Club, uliofufuliwa 2021 Bw Uhuru Kenyatta, ambaye kwa sasa ni Rais mstaafu.

“Watoto walemavu pia wanahusishwa katika upandaji miti chini ya shirika la Makele Youth Drive,” Patricia anadokeza. Mfumo huo umefaulu kwa asilimia 70 katika shule anazofanya kazi nazo.

Baadhi ya wanafunzi hufurahia kupanda miti kwa mara ya kwanza kupitia mfumo huo wa plastiki za kudondoa maji, na shule zinaandikisha mafanikio kulisha wanafunzi – kutokana na chakula wanachozalisha.

Mfumo huo unaweza kutumika kwa upanzi wa miti ya matunda, miti asilia na ya kisasa, na hata mimea mingine. Patricia anaamini kuwa lengo la serikali kupanda miti bilioni 15 kufikia 2032 linaweza kuafikiwa kupitia teknolojia kama hii rahisi ambayo pia inalinda mazingira.

Licha ya changamoto za kifedha kunogesha azma yake, Patricia anaendelea kujikaza kisabuni. Gharama ya kuunda kipande kimoja anakadiria kuwa Sh150 na kukiuza Sh250, na kila mteja hupokezwa mche wa mti.

Chini ya shirika lake, Makele Youth Drive, Patricia Makele ametoa mafunzo kwa vijana wenza kuhusu teknolojia ya chupa za sharubati kufanya kilimo. Picha|Sammy Waweru

Anahudumu na vijana wenye umri kati ya miaka 18 hadi 35, wakiwemo wasio na elimu ya vyuo vikuu, kutumia vipaji vyao kwa minajili ya kutunza na kulinda mazingira.

Kituo chake, aidha, kinahudumu na vijana 30 kwa njia ya moja kwa moja, na zaidi ya 400 kwa njia isiyo ya moja kwa moja.

Akipata uungwaji mkono na serikali ya Kaunti ya Nairobi, Patricia alishiriki Maonyesho ya Kimataifa ya Kilimo na Kibiashara Nairobi, 2024, yaliyoandaliwa na Muungano wa Ushirika wa Kilimo Kenya (ASK), ambapo alitumia jukwaa hilo kuonyesha umahiri na ubunifu wake kuboresha mazingira hasa kipindi hiki Kenya na ulimwengu unalemewa na athari za tabianchi.