Habari za Kitaifa

Tahadhari kolera ikiangamiza watu 18 katika kaunti sita

Na WINNIE ATIENO June 19th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

KENYA inapambana na mlipuko wa kipundupindu ambao umeangamiza watu 18 kufikia sasa. Waziri wa Afya, Bw Aden Duale, amethibitisha kuwepo kwa ugonjwa huo huku kaunti za Nairobi, Mombasa, Kisumu, Migori, Homabay, Kwale na Turkana zikiathirika pakubwa.

Akiongea katika mkutano wa afya huko Mombasa, Waziri huyo alisema serikali kuu imeweka mikakati kukabiliana na ugonjwa huo.

Katika kaunti ya Mombasa, watu wanne kutoka mtaa wa mabanda wa Kibarani waliaga dunia baada ya kuugua ugonjwa huo.

“Ni ukweli kuna mlipuko wa kipindupindu na kaunti kadhaa zimeathirika ikiwemo Nairobi, Mombasa, Kisumu, Migori, Homabay, Kwale na Turkana. Hata hivyo tumeweka mikakati kuudhibiti,” alisema Bw Duale kwenye mahojiano.

Alisema serikali kuu inasaidia serikali za kaunti kudhibiti ugonjwa huo usisababishe maafa zaidi.

“Tumetuma maafisa wa afya ya umma na wadadisi wa afya kukabiliana na ugonjwa huo,” alisema Waziri huyo.

Kulingana na takwimu kutoka kwa Wizara ya Afya, kuna visa 379 kote nchini.

Hata hivyo katika saa 24 zilizopita hakuna mgonjwa wa kipundupindu ameaga dunia. Kati ya walioaga dunia 13 ni wanaume, wanne ni wanawake.

Takwimu za wizara zinaonyesha Migori ikiwa na wagonjwa 53 wa kipundupindu, Nairobi (69), Kisumu (99), Kwale (48), Turkana (89) and Mombasa (21).

Kisa cha kwanza kiligunduliwa mnamo Februari 12, 2025 Kaunti ya Migori.

Vifo vilinakiliwa katika kaunti za Kisumu (1), Migori (2), Nairobi (3), Kwale (1) huku Turkana na Mombasa ikiongoza kwa vifo (4).

Bw Duale alisema wizara yake inashirikiana na washikadau katika sekta ya afya kukabiliana na mlipuko huo.