Chama cha UDA chakutana na CCM kujifunza
CHAMA tawala nchini Tanzania, Chama cha Mapinduzi (CCM), kimeanzisha mazungumzo na United Democratic Alliance (UDA) kwa lengo la kuimarisha uhusiano kati yake na chama hicho tawala nchini Kenya.
Hatua hiyo inajiri mwezi mmoja baada ya Wakenya na Watanzania kurushiana cheche za maneno kufuatia kisa ambapo wanasiasa na wanaharakati kutoka Kenya walifurushwa kutoka Tanzania huku Boniface Mwangi akizuiwa na kuteswa. Miongoni mwa waliofurushwa ni kiongozi wa chama cha People’s Liberation Party (PLP) Martha Karua na Jaji Mkuu mstaafu Willy Mutunga.
Lakini mnamo Jumatano, Juni 18, 2025, Katibu Mkuu wa CCM Emmanuel Nchimbi alifanya mazungumzo na mwenzake wa UDA, Hassan Omar Hassan jijini Nairobi.
Kwenye taarifa iliyotolewa baada ya mkutano huo, viongozi hao walisema kuwa mazungumzo yao yalikita katika njia za kuimarisha ushirikiano na mahusiano kati yao.
“Mazungumzo yalikita katika mbinu za kuimarisha mahusiano kati ya vyama vya CCM na UDA kwa manufaa ya watu wa nchi hizo rafiki na jirani,” ikasema taarifa fupi iliyotolewa na Bw Hassan baada ya mkutano huo uliofanyika katika makao makuu ya UDA, Hustler Plaza.
Chama cha CCM, kimekuwa mamlakani tangu 1961 Tanzania ilipopata uhuru, kimejijenga kisiasa nchini humo kuanzia ngazi za mashinani.
Rais Samia Suluhu Hassan ndiye mwenyekiti wa CCM na wakati huu chama hicho kinajiandaa kwa uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka huu.
Bw Omar alisema UDA inalenga kutathmini mfumo wa uongozi na asasi za CCM ikilenga kuziiga inapojijenga wakati huu inapokabiliwa na upinzani mkubwa kutoka kwa upinzani ukiongozwa na aliyekuwa naibu rais Rigathi Gachagua.
“Chama cha UDA kinalenga kuiga mifumo ambayo imeiwezesha CCM kudumisha uthabiti wake kwa zaidi ya miongo sita,” akaeleza.
Bw Nchimbi, katibu mkuu wa CCM, aliandamana na Balozi wa Tanzania humu nchini Bernard Yohana Kibesse.
Naye Bw Omar aliandamana na maafisa wa UDA akiwemo wakili wa chama hicho Adrian Kamotho.
Mnamo Februari mwaka huu, Bw Omar aliongoza ujumbe wa maafisa wa UDA kufanya mkutano na maafisa wa chama tawala nchini Uganda, National Resistance Movement (NRM).
Awali, chama cha UDA pia kimewahi kufanya mazungumzo na ujumbe kutoka chama cha Kikomunisti cha China (CCP), kujifunza kuhusu mbinu bora za kudumisha usimamizi wa asasi zake.