Siasa

Maagizo magumu ya Rais Ruto kwa Baraza la Mawaziri

Na RUSHDIE OUDIA June 22nd, 2025 Kusoma ni dakika: 3

RAIS William Ruto ameagiza mawaziri kuharakisha utekelezaji wa miradi muhimu anayotaka ikamilike kabla ya mwisho wa muhula wake wa kwanza, huku kila waziri akitakiwa kuwasilisha mpango kamili wa utekelezaji ndani ya wiki mbili.

Akiongoza kikao maalum cha siku mbili cha viongozi wakuu wa serikali eneo la Karen, Nairobi, Rais Ruto alisisitiza kuwa utekelezaji wa miradi hiyo ni lazima na hakuna kufeli.

Naibu Rais Kithure Kindiki naye alielekeza wizara, idara na mashirika ya serikali kuwasilisha mapendekezo na mpango wa utekelezaji wa miradi ya serikali ndani ya siku 14, ili ikamilike ndani ya kipindi kilichosalia cha miaka miwili na nusu cha utawala wa Kenya Kwanza.

Wakati wa kufunga kikao hicho, Rais Ruto aliwataka maafisa wakuu wa serikali kuwajibika zaidi hasa katika mchakato wa ununuzi serikalini.

“Kuanzia Julai 1, ununuzi wote wa serikali utatekelezwa kupitia mfumo wa kielektroniki. Hili si ombi, ni agizo kwa maafisa wote wa fedha ili kuzuia wizi na kupunguza gharama zisizo halali katika shughuli za ununuzi serikalini,’ alisema Rais Ruto.

“Ununuzi serikalini lazima uwe wa wazi kabisa. Lazima tujue ni nani waliowasilisha zabuni, nani alishinda, na ni kiasi gani kilichotolewa.”

Licha ya juhudi za awali chini ya utawala wa Rais mstaafu Uhuru Kenyatta kuanzisha mfumo huo, hakuna hatua madhubuti zilizopigwa. Sasa macho yote yanaelekezwa kwa Rais Ruto na timu yake, huku zikibakia siku nane utekelezaji uanze.

Rais Ruto pia alieleza kuwa maafisa wa umma watawajibikia binafsi matumizi mabaya ya fedha za wananchi hususan ununuzi wa kiholela.

“Ili kuepuka yaliyoibuliwa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali katika ripoti zake, Wizara ya Fesha kwa ushirikiano na Mkuu wa Utumishi wa Umma inapaswa kutoa ilani kuimarisha kanuni na kuhakikisha kuna uwajibikaji wa moja kwa moja kwa maafisa wanaohusika,’ alisema Ruto.

Aliongeza: “Unakuta afisa wa umma anatoa zabuni ya vifaa vya hospitali ilhali jengo lenyewe halijajengwa. Mwisho wa siku ni pesa kupotea na mzigo ni kwa mlipa ushuru.”

Changamoto zilizotambuliwa kwenye kikao hicho ni pamoja na kesi mahakamani, mabadiliko ya kisiasa ya kimataifa, upungufu wa bajeti, na taarifa potofu kupitia mtandao.

“Tuliona mafanikio katika baadhi ya maeneo muhimu, lakini pia kulikuwa na mapungufu yanayopaswa kushughulikiwa ili serikali itimize mkataba wake na wananchi,” ilisema taarifa rasmi ya kikao hicho.

Kuimarisha ufanisi na imani ya wananchi kwa serikali, Rais alitaja mambo kadha ambayo yamepewa kipaumbele.

Kuongeza akiba ya fedha za kigeni kupitia ongezeko la mauzo ya nje; kujenga vituo vya teknolojia za habari na mawasiliano (ICT) kote nchini; kununua kompyuta za kuendesha vituo hivyo; na kuhakikisha ununuzi wa serikali unashirikisha wizara zote.

Katika sekta ya kilimo Ruto alisisitiza haja ya kuboresha takwimu katika sekta ndogo za kilimo ili kuwezesha maamuzi yanayoimarisha uzalishaji, mapato na ajira.

Kuhusu elimu serikali inapanga kuajiri walimu zaidi ili kuimarisha idadi ya mgao wa walimu kwa wanafunzi, na kuendelea kukuza mfumo mpya wa Elimu ya Umilisi na Utendaji(CBC). Serikali pia inalenga kuboresha mfumo wa kufadhili elimu ya vyuo vikuu kwa kuhakikisha kila mwanafunzi anaorodhesha katika kundi sahihi kulingana na uwezo wake wa kifedha.

Kuhusu afya, serikali itaendelea na juhudi za kusajili Wakenya wote katika Bima ya Afya ya Jamii (SHIF) ili kila mwanachi apate huduma bora.

Kikao pia kilitambua mwelekeo mpya wa kisiasa baada ya kuundwa kwa Serikali Jumuishi kufuatia makubaliano kati ya United Democratic Alliance (UDA) na Orange Democratic Movement (ODM).

Pia, kuna mpango wa kujenga maabara na miundombinu muhimu kuboresha shule zote nchini ili kutoa elimu bora kwa wote.

Serikali pia inalenga kuboresha mfumo wa kufadhili elimu ya vyuo vikuu kwa kuhakikisha kila mwanafunzi anaorodhesha katika kundi sahihi kulingana na uwezo wake wa kifedha.

Kuhusu afya, serikali itaendelea kusajili Wakenya wote katika Hazina ya Bima ya Afya ya Jamii ili kuhakikisha kila mmoja anapata huduma boraKikao pia kilitambua mwelekeo mpya wa kisiasa baada ya kuundwa kwa Serikali Jumuishi kufuatia makubaliano kati ya United Democratic Alliance (UDA) na Orange Democratic Movement (ODM).