Suala la upangaji uzazi asilia katika ndoa
UPANGAJI uzazi asilia ni mbinu ya kupanga uzazi inayohusisha kufuatilia dalili za asili za mwezi wa uzazi wa mwanamke ili kubaini kipindi cha kupata au kuepuka ujauzito.
Steve Musamali, mtaalamu na mtafiti wa masuala ya upangaji uzazi asilia, anafafanua kuwa njia hii huwasaidia wanandoa kuamua muda wa kupata ujauzito au kuzuia kwa kutumia maarifa ya mwili wa mwanamke.
Kwa mujibu wa Bw Musamali, njia hii inahusisha kuelewa mwezi wa uzazi wa mwanamke yaani kipindi ambacho anaweza kupata ujauzito au kuepuka.
“Kuna ule wakati mwanamke ana uwezekano mkubwa wa kushika mimba, hasa wakati wa mchakato wa kuachilia yai la kike kwenye mkondo wa uzazi,’ anaeleza.
Katika mwezi wa uzazi wa mwanamke wa kawaida wa siku 28, wakati wa mchakato wa kuachilia yai la kike kwenye mkondo wa uzazi hutokea katikati kwa mfano, siku ya 14.
Bw Musamali anaeleza kuwa mwezi wa uzazi wa baadhi ya wanawake huwa katika makundi ya siku 26, 28, au 32.
Ili kubaini siku zako, mzunguko hugawanywa mara mbili. Hii inamaanisha katika mzunguko wa siku 28, yai huachiliwa kati ya siku ya 14 hadi 15.
Kipindi cha kushika ujauzito basi huwa kati ya siku ya tisa hadi 16 kwa sababu mbegu za kiume zinaweza kuwa hai mwilini kwa siku tano, huku yai likiwa na uhai wa saa 24 hadi 48.
Njia za upangaji uzazi asilia ni pamoja na kufuatilia kalenda, mabadiliko ya joto la mwili, kufuatilia ute wa ukeni (Cervix mucus).
Bw Musamali anasisitiza umuhimu wa kufuatilia dalili hizi hasa kwa wanawake walio na mizunguko ya mwezi wa uzazi wa kawaida.
Faida za upangaji uzazi asilia, Bw Musamali anaeleza kuwa faida ya kwanza ya aina hii ya upangaji uzazi ni kuwa haina madhara.
“Njia hii haina athari za kiafya zinazohusiana na vidonge au mbinu za kisasa.”
Mbinu hii pia haina gharama yoyote kwani haihitaji matumizi ya vifaa vya gharama kubwa.Kando na hayo, anasema kuwa mbinu hii husaidia kuimarisha uhusiano.
“Wanandoa wanapojifunza na kufuatilia kalenda pamoja, huongeza mawasiliano na mshikamano.”
Isitoshe, anasema kuwa mfumo huu husaidia wanawake kuelewa miili yao na kubaini matatizo ya kiafya kama vile mizunguko isiyo ya kawaida au changamoto za uzazi.
Hata hivyo, Bw Musamali anatahadharisha kuwa njia hii inafaa zaidi kwa wanawake wenye mizunguko ya kawaida.
Kwa jumla, upangaji uzazi asilia ni njia salama, ya asili, na inayowezesha wanandoa kufanya maamuzi ya uzazi kwa maarifa na uwazi zaidi.