Maswali mshukiwa mwingine akifariki saa chache baada ya kukamatwa Nyandarua
KIFO cha kutatanisha cha mshukiwa aliyekuwa kizuizini katika Kituo cha Polisi cha Turasha, Kaunti ya Nyandarua, saa chache baada ya kukamatwa, kimezua ghadhabu miongoni mwa wakazi wanaotaka haki itendeke mara moja.
Polisi wanadai kuwa mshukiwa huyo alijitia kitanzi, lakini hali ilivyo imeibua maswali mengi, hasa baada ya kubainika kuwa jina lake liliandikishwa visivyo katika kitabu cha matukio (OB).

Bw Simon Tumbi Kihanya, mwenye umri wa miaka 44, alikamatwa Jumatatu mchana akiwa njiani kuelekea soko la Turasha.
Kwa mujibu wa polisi, alikutwa akiwa na koti linalodaiwa kuwa na uhusiano na mfanyabiashara anayeaminika kuhusika na ulanguzi wa bangi.
Hata hivyo, jina lake lilisajiliwa kama “Ruigi Ndubi” kwenye OB Nambari 6/23/6/2025, na alishtakiwa kwa kosa la kuwazuia polisi kutekeleza majukumu yao.
Habari za kifo chake jioni hiyo zilichochea maandamano katika kituo hicho cha polisi.