Milipuko ya vitoa machozi maandamano yakichacha miji mkuu nchini
MLIPUKO mikubwa inasikika katikati ya jiji la Nairobi polisi wakifyatulia vitoa machozi waaandamanaji wanaoadhimisha kuuawa kwa vijana zaidi 60 mwaka jana wakipinga mswada wa Fedha 2024.
Maandamamo hayo yanaendelea katika miji zaidi ya 16 kote nchini. Vijana wamemiminika katikati ya jiji licha polisi kuweka vizuizi kuthibiti magari na wanaoingia jijini.
Wakati mmoja waandamanaji walijaribu kuvamia kituo cha polisi cha Central lakini wakatawanywa kwa vitoa machozi. Maandamano yamechacha Githurai, Kitengela, Mlolongo, Nyeri, Nakuru, Karatina,Mombasa, Nyahururu, Wote miongoni mwa miji mingine.
Shughuli zote zimesimama katikati ya miji na mitaa ambako wakazi wanaandamana.
Vijana na baadhi ya viongozi wa upinzani Kalonzo Musyoka, David Maraga na Eugene Wamalwa walipenya katikati ya jiji licha usalama kuimarishwa na kujiunga na waandamanaji.
Mbunge wa Embakasa Mashariki Babu Owino na Seneta wa Busia pia walionekana barabarani wakiungana na waandamanaji waliokuwa wakiimba nyimbo za kukashifu serikali na kutaka haki.
Usalama ulikuwa umemarishwa vikali katika jiji la Nairobi kuanzia asubuhi Jumatano Juni 25, huku maafisa wa polisi wakifunga barabara kuu zinazoelekea katikati ya jiji (CBD), katika maandalizi ya maandamano yanayoendelea. Hali hii ilibabisha usumbufu mkubwa kwa waliotaka kufika katikati ya jiji.
Hata hivyo, vijana walifaulu kufika kati kati ya jiji na kuanza maandamano huku maduka yakifungwa na magari yakiwa machache sana.
Polisi waliweka vizuizi na kuanza kukagua magari, huku wakidhibiti kabisa yanayoingia katikati ya jiji. Magari ya usafiri wa umma yaliathiriwa zaidi, na abiria kulazimika kushuka mbali na katikati ya jiji na kutembea kwa miguu.
Barabara za Parliament Road, Harambee Avenue na Kenyatta Avenue zilifungwa kabisa, na maafisa wa usalama wameweka waya wa miiba pamoja na vizuizi vingine. Maandamano haya ni kumbukumbu ya hali iliyoshuhudiwa wakati wa maandamano Juni 25 mwaka jana.