Habari za Kitaifa

Raila azomewa na wabunge, alazimika kukatiza hotuba kikao cha Serikali Jumuishi

Na CECIL ODONGO, DAVID MWERE August 19th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

KINARA wa ODM Raila Odinga jana alizomewa na wabunge ambao walieleza kukerwa na shinikizo zake kuwa wapokonywe Hazina ya Ustawishaji wa Maeneobunge (NG-CDF).

Rais William Ruto naye hakusazwa, wabunge wakimkaba koo na kudai anawaandama kwa tuhuma za kupokea hongo ilhali wamekuwa wakikabiliwa na hali ngumu kutetea utendakazi duni wa serikali yake kwa raia.

Rais Ruto na Bw Odinga jana walikuwa wameongoza mkutano wa wabunge wa ODM na wale wa Kenya Kwanza mtaani Karen, Nairobi.

Hasira zililipuka licha ya mkutano huo kutarajiwa kutumika kunogesha ushirikiano wa vyama vya UDA na ODM hasa kuhusu uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2027.

Bw Odinga alikuwa akihutubu kuhusu jukumu la wabunge la kufuatilia utendakazi wa serikali na kutetea kaunti zipewe CDF, wabunge waliponung’unika na kumzomea licha ya kujitahidi kutoa ufafanuzi.

“Kazi ya bunge ni uwakilishi, kutunga sheria na kutathmini utendakazi. Hilo ni wazi. Bunge halifai kutekeleza, Bunge linafaa kutia kwenye mizani,” Raila akasema huku wabunge wakiingilia kati na kumvuruga.

Rais Ruto ambaye alikuwa ameketi chini pamoja na wote waliohudhuria, alionekana akiuelekeza mkono wake nyuma na kuashiri wabunge wasimzomee Bw Raila.

Bw Odinga aliyeonekana kukerwa na hatua ya wabunge hao, aliwaambia kuwa watakuwa na nafasi ya kusema kauli zao na kujibu msimamo wake.

“Ninaomba mnisikilize kisha mtakuwa na nafasi ya kujibu,” akasema Bw Raila akionekana kutikiswa.

Bw Raila aliwakera wabunge hao zaidi alipodai kuwa wao hupokea hongo kutoka kwa maafisa wa serikali ambao wanafika mbele yao ili waandike ripoti zinazowaondolea lawama kuhusu madai mbalimbali.

Bw Raila amekuwa akipinga wabunge kusimamia CDF akisema hazina hiyo inastahili kusimamiwa na magavana.

Mbunge wa Rarieda Otiende Amollo ambaye ni mwandani wa Bw Raila ndiye alikuwa mdhamini wa mswada ambao unahakikisha CDF inawiana na Katiba ya 2010 ili isalie mikononi mwa wabunge.

Pendekezo la Bw Raila la kuwapokonya wabunge CDF pia limepata upinzani mkali kutoka kwa raia ambao wamesifia jinsi hazina hiyo ilivyowakwamua watu maskini hasa kielimu.

Aliposimama kuhutubu, Rais Ruto naye hakusazwa huku wabunge wakimtaka azungumzie madai yake ya kuwa wanapokea hongo aliyoyatoa akiwa Homa Bay wakati wa Kongamano la Ugatuzi.

Wabunge hasa walimtaka ataje wale ambao amekuwa akisema walipokea hela hizo.

“Sitawataja na kuwaaibisha hapa, tutawakamata,” akasema Rais huku akifunguka moyo na kusema wao hupata pesa hizo kutoka kwa magavana.

“Niambieni unatoa wapi Sh150 milioni? Hizo ni pesa za kaunti. Wabunge walipokea hongo ya Sh10 milioni kupitisha Mswada wa Utakatishaji wa Pesa,” akaongeza Rais Ruto.

“Si mlipata pesa? Mnakusanya pesa kisha kugawana nyie watu wachache na kuharibu maadili ya bunge,” akasema akionekana pia kukabiliana na manung’uniko ya wabunge.

Baadhi ya wabunge ambao hawakutaka kunukuliwa walisema ni utovu wa maadili kuzomewa na Raila na Rais Ruto kama watoto wadogo ilhali wamekuwa wakitetea serikali kwa Wakenya.

“Hawatafaulu wakichukua huo mkondo wa kuwaandama wabunge na hatutakubali. Kama wanataka kubadilisha uongozi bunge waseme tu badala ya kutumia mianya na njia za mkato,” akasema mbunge mmoja aliyekataa kutajwa.

Mkutano wa jana uliishia kwa hasira wala mapendekezo yaliyoafikiwa hayakusomwa.