Habari

Kenya kutengeneza mbolea yake, Ruto asema

Na ERIC MATARA November 4th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

KENYA itapunguza kiasi cha mbolea inayoagizwa nje ya nchi na kuanza kutengeneza bidhaa hiyo nchini ili kuwawezesha wakulima kuinunua kwa bei nafuu.

Hii ni baada ya Rais William Ruto kuzindua mradi wa Sh100 bilioni wa kutengeneza mbolea eneo la Olkaria Naivasha Jumatatu Novemba 3, 2025.

Mradi huo unatekelezwa na Kampuni ya Kaishan kutoka China na Kampuni ya Kutengeneza Kawi ya Mvuke (KENGEN).

“Kama nchi, tunatumia hela nyingi kuagiza mbolea kutoka nje ya nchi. Hata hivyo, hivi karibuni tutapunguza kwa sababu tutakuwa tukizalisha mbolea yetu. Kiwanda hiki cha kutengeneza mbolea cha KenGen-Kaishan kitahakikisha kuwa tuna mbolea ya kutosha,” akasema Rais Ruto.

“Kutegemea mbolea inayoagizwa hupandisha bei na kusababisha wakulima waumie kwa sababu ya kupanda kwa bei kwenye soko la kimataifa ambalo huathirika na mambo mengi ikiwemo vita vya Urusi-Ukraine,” akaongeza Rais Ruto.

Kwa mwaka wa pili mfululizo, mbolea ambayo inaagizwa na serikali imepungua hali inayoashiria kuwa mpango wa serikali wa kutoa mbolea kwa bei nafuu kwa wakulima huenda ukaathirika.

Shirika la Kitaifa la Takwimu Nchini (KNBS) zinaonyesha kuwa Kenya iliagiza tani 443,701 za mbolea kati ya Januari na Juni 2025 , kiwango ambacho kiligharimu Sh25.63 bilioni. Huu ulikuwa upungufu kutoka tani 445,857 wa thamani ya Sh27.71 bilioni kipindi hicho mwaka jana.

Ukikamilishwa, mradi huo wa Olkaria utazalisha tani 480,000 za mbolea kila mwaka. Rais alisema kiasi hicho kitasaidia kuwakinga wakulima kutoka bei zisizotabirika za mbolea katika soko la kimataifa.

“Changamoto za mbolea zimechangia kuongezeka kwa bei ya vyakula, zikapunguza uzalishaji na kupunguza mapato ya wakulima,” akasema.
Mnamo 2023 Kenya iliagiza mbolea zaidi ya tani 600,000 na tani 443,000 katikati mwa 2025 kwa kima cha Sh60 bilioni.

“Kila shehena ya mbolea inayosafirishwa inanyima wakulima wetu nafasi. Shughuli ya leo itahakikisha kwamba tunazalisha mbolea yetu,” akasema kiongozi wa nchi.

Mradi huo utatumia megawati 165 ya umeme wa mvuke kubadilisha ammonia kijani hadi mbolea, Rais akisema ni mradi wa aina yake na wa kwanza Afrika.
Rais alikuwa ameandamana na Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi, Mkurugenzi wa Kaishan Dkt Yang Tang, na Afisa Mkuu Mtendaji wa KenGen Peter Njenga pamoja na wabunge kadhaa pamoja na viongozi wengine.

Rais aliongeza kuwa mradi huo utapunguza kiasi cha kaboni inayoachiliwa hewani kwa zaidi ya tani 600,000.

“Mradi huu utabuni nafasi 200,000 za ajira kila mwaka kwa kipindi cha miaka miwili ambacho ujenzi utakuwa ukiendelea. KenGen nayo itakuwa ikipata faida ya Sh1.7 bilioni kila mwaka,” akasema Rais Ruto.