Makundi mbalimbali kupokea mafunzo ya kuyasaidia kuboresha biashara zao
MAMLAKA inayosimamia Biashara Ndogo-ndogo (MSEA), imeanzisha rasmi mpango wa kutoa mafunzo kwa wafanyabiashara kuhusu masuala ya kuboresha biashara zao ili kuwawezesha kuinuka kiuchumi.
Mradi huo wa Kenya Jobs and Economic Transformation (KJET) unalenga makundi 94 ya biashara nchini.
Mafunzo hayo ya awamu ya kwanza yalianza Novemba 10, 2025, na yanaendeshwa katika kaunti 10 kabla ya kufikia kaunti zote 47 katika kipindi cha wiki tano zijazo.
Mafunzo hayo yanalenga kuboresha uzalishaji na ukuaji katika sekta ya MSMEs).
Kupitia mitaala ya moduli 12, wahusika wataweza kujenga ujuzi wao wa kutenda kazi utakaowasaidia kuongeza tija, kuimarisha ushindani na kufikia masoko mapya.
Mafunzo hayo yanajumuisha mazoezi, mifano halisi na kazi za makundi zinazoongozwa na wakufunzi waliobobea.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mafunzo hayo Nairobi, Mkurugenzi Mkuu wa MSEA, Bw Henry Rithaa, alisema mradi huo unalenga kuoresha MSMEs ili iwe injini ya ubunifu, ajira na ukuaji shirikishi wa kiuchumi.
Baada ya mafunzo, makundi hayo yataendelea na awamu ya pili itakayojumuisha mafunzo ya miezi mitatu na ushauri wa karibu kutoka kwa wataalamu ili kusaidia utekelezaji wa mafunzo.