Gachagua: Malala hajahama DCP; tumekamilisha mpango wa Wantam
ALIYEKUWA Naibu Rais Rigathi Gachagua amesema kuwa wamekamilisha kubuni mikakati ya kumfurusha Rais William Ruto 2027 na watakuwa wakitembelea kila eneo kuwaeleza siri hizo.
Alikanusha vikali kauli ambayo imekuwa ikitolewa mara kwa mara na Rais William Ruto kuwa upinzani hauna ajenda na mbinu ya kumbandua madarakani, akiapa kuwa watamwonyesha kivumbi mnamo 2027.
“Kila kitu kimekamilika na tutakuwa tukizuru maeneo mbalimbali kuwaonyesha Wakenya mpangilio wetu wa maendeleo na mbinu za kumngátua,” akasema Bw Gachagua akihutubia vyombo vya habari jijini Mombasa.
Aliorodhesha usajili wa wapigakura na kukabiliana na kile alichotaja kama uongo wa Rais Ruto kama mkakati wa tatu wa kupambana na utawala wake.
Hatua ya nne itakuwa kuwashaajisha wapigakura wajitokeze kwa wingi kumwondoa Rais kupitia uchaguzi kisha mkakati wa tano utakuwa upinzani kulinda kura zake.
Mikakati miwili itakayosalia ni kukabiliana na Rais kupitia Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC) na kortini baada ya kumbwaga uchaguzini kisha mwishowe “waanze utawala wao.”
Kuhusu madai kwamba kambi yake inaendelea kutorokwa na waliokuwa wandani wake, Bw Gachagua amesema hana wasiwasi kwa sababu la muhimu ni kuwa na uungwaji mkono wa raia.
“Rais Ruto ndiye anastahili kuingiwa na uoga hasa akijua wanasiasa ambao wanadai ni wandani wake na wanapanga kumhepa kuja upinzani. Azma yake ya 2027 hivi karibuni itakuwa pabaya,” akaongeza.
Ni katika mahojiano hayo ambapo alikanusha kwamba Naibu Kiongozi wa DCP Cleophas Malala amegura kambi yake akisema seneta huyo wa Kakamega amelemewa na mafua.
“Mabloga wa Ruto ni watu wa ajabu na wale ambao wanaondoka DCP hawakuwa watu wetu. Iwapo wewe ni fuko ndani ya DCP ondoka kabla tukuondoe na wale wanaoondoka kwa sababu tumekataa ombi lao la kupewa tikiti moja kwa moja pia nao waende mahali watapendelewa,” akasema.
Kauli hiyo inaonekana ilimlenga Mbunge wa Juja George Koimburi ambaye alihama DCP wiki jana akidai Bw Gachagua anawatapeli wanasiasa hela kwa ahadi ya kupata tikiti ya chama hicho.
Hata hivyo, aliyekuwa naibu rais alisema kujiunga au kuondoka ndani ya chama cha kisiasa ni jambo la kawaida.
Kuhusu siasa za Pwani, kiongozi huyo alisema upinzani ushaamua kumuunga mkono Mbunge wa Nyali Mohamed Ali awanie ugavana 2027.
“Tumekubaliana na Kalonzo kumuunga mkono ila kile ambacho hatujakubaliana ni chama kipi atakachotumia 2027 kati ya Wiper na DCP,” akasema.
Alimrejelea Bw Ali ambaye amehudumu mihula miwili bungeni, kama kiongozi mchapakazi, mshikilia dini na asiyekuwa na doa la ufisadi.
Pia aliahidi kwamba atapambana na tatizo la matumizi ya mihadarati ambalo limepiga kambi eneo la Pwani kwa miaka mingi.
Alidai baadhi ya wanasiasa kutoka Pwani ni walanguzi wa dawa za kulevya na wamepiga vita juhudi za kutokomeza tatizo hilo kwa sababu wanahudumu serikalini.
“Tukiunda serikali walanguzi wa dawa za kulevya watafungwa na kuuza dawa hizo kutakuwa haramu nchini. Hospitali zote za Level Four zitakuwa na idara ya urekebishaji tabia,” akasema.