Makala

DPP aamuru maafisa waliompiga risasi na kumuua mwanaume wa miaka 20 washtakiwe

Na RICHARD MUNGUTI January 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MKURUGENZI wa Mashtaka ya Umma (DPP), Renson Ingonga ameamuru maafisa wawili wa polisi waliompiga risasi na kumuua mwanaume wa miaka 20 katika eneo la Mukuru kwa Njenga washtakiwe kwa mauaji.

Sajini Godwin Mjomba na Konstebo Patrick Mutunga Titus watafikishwa mbele ya Jaji katika Mahakama kuu ya Milimani Ijumaa mnamo Januari 30,2026 kujibu shtaka la kumuua Shukri Adan mnamo Januari 11,2026.

DPP alitoa agizo hilo baada ya kusoma ushahidi uliokusanywa na wachunguzi wa mauaji hayo ya Adan siku 20 zilizopita.

“Baada ya kutathmini ushahidi uliowasilishwa na wachunguzi nimefikia uamuzi kwamba Sajini Mjomba na Konstebo Mutunga washtakiwe kwaa mauaji ya Shukri Adan,” DPP alieleza hakimu mwandamizi Carolyne Mugo.

Hakimu aliombwa aamuru Saj Mjomba na Konstebo Mutunga wazuiliwe katika kituo cha polisi cha Capitol kabla ya kufikishwa mbele ya Jaji kujibu shtaka la mauaji.

Wawili hao walifikishwa kortini Januari 12,2026 baada ya kumpiga risasi Shukri.

Polisi waliomba washukiwa hao wa mauaji wazuiliwe kwa siku 14 lakini Bi Mugo akaamuru wazuliwe siku 10.

Akiamuru wawili hao watupwe rumande Bi Mugo alisema mauaji ya Shukri Adan Ibrahim Issaka Januari 11,2026 yalikera umma na kusababisha maandamano na uharibifu wa mali.

Hakimu alikubaliana na mamlaka huru ya polisi IPOA iliyochunguza kesi hiyo kwamba sharti uchunguzi wa kina ufanywe kubaini sababu ya Shukri kuuawa kinyama.

Naibu Mkurugenzi wa Masuala ya Uchunguzi IPOA Abdirahaman Jibril alimweleza hakimu kwamba kulikuwa na njama kuvuruga uchunguzi na kuficha mauaji hayo ya Shukri.

Maafisa wa polisi kutoka kituo cha Villa kilichoko eneo la Mukuru kwa Njenga eneo la Embakasi kaunti ya Nairobi walidaiwa kuimbuka na njama hiyo ya kuwaficha wenzao.

Shukri aliuliwa katika eneo la MCC mwendo wa saa 12 na dakika 10 asubuhi.

Kabla ya kuuawa Shukri, mahakama ilielezwa alikuwa ameandamana na Wycliffe Nyakwama na Festus Mutinda.

Watatu hao walikuwa wanaipeleka gari namba ya usajili KDN 266B muundo wa Toyota Fielder kwa Bw Joho katika mtaa wa Imara Daima.

Wakiwa njiani mahakama iliambiwa gari hilo liligongana na gari ya Matatu ndipo vurumai na mtafaruku vikazuka.

Mahakama ilielezwa ni wakati huo maafisa hao polisi walifika na kuwaamuru Shukri , Nyakwama na Mutinda walale chini.

“Shukri alipigwa risasi ya kichwa na kufa papo hapo,” Jibril alieleza mahakama.

Mwili wa Shukri ulichukuliwa na wananchi na kupelekwa katika msikiti ulioko Mukuru kwa Njenga kwa maombi na hatimaye akazikwa baada ya kufanyiwa upasuaji kubaini kiini cha kifo.

Jibril aliomba washukiwa hao wazuiliwe kwa siku 21 kuwezesha IPOA kukamilisha uchunguzi.

Washukiwa hao walipinga kusukumwa jela siku 14 wakisema wameshirikiana na wachunguzi wa IPOA.

Akiamuru polisi hao wazuiliwe rumande hakimu alisema wapelelezi wanahitaji kukamilisha zoezi na kuwahoji mashahidi.

Hakimu alisema wawili hao sharti wapelekwe kupimwa ikiwa akili zao ni timamu kuwezesha washtakiwe kwa mauaji.