Upinzani warudia sumu iliyouponza mwaka jana
HUKU chaguzi ndogo katika wadi za Muminji, Evurore, Kabras West na eneo bunge la Isiolo Kusini zikikaribia, dalili zinaonyesha kuwa huenda upinzani uko njiani kurudia makosa yaliyofanya ushindwe katika chaguzi ndogo za mwaka jana.
Badala ya kujifunza kutokana na fedheha ya chaguzi ndogo za Novemba 2025, upinzani unaonekana kuangukia tena mtego wa ushindani wa ndani, vita vya ubinafsi na kukosa uratibu wa kimkakati. Hali hii imeibua wasiwasi miongoni mwa wachambuzi wa siasa wanaosema historia iko mbioni kujirudia.
Mchanganuzi wa masuala ya kisiasa, James Warukira, tatizo kuu la upinzani ni kushindwa kutambua kuwa chaguzi ndogo huhitaji mshikamano wa hali ya juu kuliko uchaguzi mkuu.
“Upinzani unaendelea kudharau nguvu ya serikali katika chaguzi ndogo. Bila umoja, hata ujumbe mzuri wa kisiasa hauwezi kushinda serikali,” asema Warukira.
Katika chaguzi ndogo za awali, upinzani ulishindwa licha ya kauli nzito za kisiasa. Aliyekuwa naibu rais Rigathi Gachagua alijitangaza kinara wa Mlima Kenya, lakini mgombea aliyemuunga mkono alishindwa, hali iliyovunja simulizi lake kwamba anadhibiti ukanda huo na kufichua udhaifu wa miundo ya upinzani.
Mtaalamu wa siasa, John Ojwang’, anasema kauli za kisiasa zisizoandamana na mipango thabiti ndizo zinaweza kuangusha upinzani.
“Upinzani hupenda kelele na matamshi makubwa, lakini hupuuza kazi ya msingi ya kupanga, kugawana maeneo na kusimamia nidhamu ya vyama,” anasema Ojwang’.
Katika wadi ya Kabras West, vyama vya DAP-K na DCP tayari vimewasimamisha wagombea tofauti dhidi ya mgombea mmoja wa UDA. Wachambuzi wanasema huu ni mfano dhahiri wa kura za upinzani kugawanyika na kupatia chama tawala ushindi wa mapema.
Mchanganuzi wa siasa za vyama, Moses Walila, anasema upinzani bado haujaelewa somo katika kutengeana maeneo kulingana na umaarufu.
“Hii si hisani, ni mkakati wa kisiasa. Ukikosa, unajitolea kushindwa. Upinzani unapuuza mikakati rahisi inayoweza kusaidia kushinda,” asema Walila.
Katika Evurore, hali si tofauti. Vyama kadhaa vya upinzani vimewsimamisha wagombea dhidi ya mmoja wa UDA. Hali hii, kulingana na wachambuzi, inapatia chama tawala faida kubwa hata kabla ya kampeni kushika kasi.
Kwa mujibu wa mchambuzi wa masuala ya utawala, Glady’s Njeri, chaguzi ndogo hupimwa zaidi kwa nidhamu kuliko umaarufu.
“Serikali huwa tayari mapema, hutumia rasilmali na mtandao wake kikamilifu. Upinzani ukiwa na wagombea wengi, unafanya kazi ya serikali kuwa rahisi,” anasema Njeri.
Wachambuzi wanakubaliana kuwa iwapo upinzani hautabadilisha mkondo wake kwa dharura, chaguzi ndogo zijazo zitakuwa marudio ya aibu ya mwaka jana. Siasa, wanasema, hulipa mshikamano, nidhamu na maandalizi ya mapema.
Bila misingi hiyo, huenda upinzani ukagundua tena kuwa kuungana kwa jina pekee hakutoshi kushinda uchaguzi.