Jamvi La Siasa

Malkia wa sheria Faith Odbiambo sasa aanza mbio za siasa

Na MWANDISHI WETU July 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Rais wa Chama cha Wanasheria nchini (LSK), Faith Odhiambo, ameonyesha wazi kuwa sasa yuko tayari kuingia kikamilifu katika siasa baada ya kujitokeza hadharani kwenye mkutano wa Linda Mwananchi uliofanyika Ijumaa mjini Kisii, hatua iliyozidi kuimarisha tetesi za kuwania kiti cha Mwakilishi wa Wanawake wa Nairobi katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Odhiambo, ambaye kwa miaka ya hivi karibuni amekuwa sauti maarufu ya kutetea Katiba, haki za binadamu na utawala wa sheria, alionekana jukwaani pamoja na aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino na viongozi wengine wa mrengo wa Linda Mwananchi.
Mkutano huo ulitafsiriwa na wengi kama hatua ya kwanza ya Odhiambo kujijenga kisiasa, hasa baada ya kupata uungwaji mkono wa Gavana Orengo, ambaye amekuwa akimsifu kama mmoja wa viongozi wanaoweza kuleta mageuzi nchini.
Kuonekana kwake katika mkutano huo kumemweka rasmi kwenye ramani ya siasa za upinzani huku kukiongeza ushindani wa kumrithi Esther Passaris, ambaye amekuwa Mwakilishi wa Wanawake wa Nairobi kwa mihula miwili.
Kwa muhula wake akiwa Rais wa LSK, Odhiambo alijitokeza kama mmoja wa wakosoaji wakuu wa serikali kuhusu masuala ya ukiukaji wa Katiba, matumizi mabaya ya mamlaka na haki za raia. Mara nyingi aliongoza vita vya kisheria kupinga hatua alizodai zilikiuka sheria, jambo lililomjengea umaarufu mkubwa kitaifa.
Sasa anatafuta kuhamisha ushawishi huo kutoka mahakamani hadi kwa wapigakura wa Nairobi, akijinadi kama kiongozi anayezingatia uwajibikaji, utawala bora na huduma kwa wananchi.
Hata hivyo, safari yake haitakuwa rahisi.
Anakutana na ushindani mkali kutoka kwa wanasiasa waliokwisha jijengea misingi ya kisiasa jijini Nairobi.
Aliyekuwa Seneta wa kuteuliwa Millicent Omanga, aliyeshindwa na Passaris katika uchaguzi wa mwaka 2022, tayari ametangaza nia yake ya kuwania kiti hicho tena. Anaaminika kuwa na mtandao mkubwa wa wafuasi na anaweza kupata uungwaji mkono kutoka kwa kiongozi wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP) alichohamia majuzi.
Pia yupo Seneta wa kuteuliwa Karen Nyamu, ambaye amedokeza kuwa atalenga kiti hicho kupitia chama cha UDA. Nyamu anategemea umaarufu wake mkubwa katika mitandao ya kijamii na ushawishi wake miongoni mwa vijana.
Seneta mwingine wa kuteuliwa Tabitha Mutinda naye ametajwa kuwa miongoni mwa wanaowania nafasi hiyo huku akijitambulisha kama kiongozi anayesisitiza maendeleo.
Majina mengine yanayotajwa ni ya Seneta wa kuteuliwa Crystal Asige, mwanaharakati Hanifa Adan na mwanablogu Maverick Aoko.
Hata hivyo, wachambuzi wa siasa wanaona kuingia kwa Faith Odhiambo kunaweza kubadilisha kabisa mwelekeo wa ushindani huo.
Tofauti na wapinzani wake waliopitia siasa za kawaida, Odhiambo anategemea rekodi yake katika taaluma ya sheria, utetezi wa haki za binadamu na mapambano dhidi ya ukiukaji wa Katiba ili kuwashawishi wapigakura.
Changamoto yake kubwa sasa ni kubadilisha umaarufu wake wa kitaifa kuwa mtandao imara wa kisiasa utakaoweza kushindana na mashine za kisiasa za wapinzani wake.
Mbio za uwakilishi wa wanawake Nairobi sasa zimegeuka kuwa pambano litakaloonyesha iwapo wapigakura wataendelea kuwaamini wanasiasa waliokomaa au watawapa nafasi viongozi wapya wanaobeba ajenda ya mageuzi.
Kwa sasa, kuonekana kwa Faith Odhiambo katika mkutano wa Linda Mwananchi mjini Kisii kumethibitisha kuwa “malkia wa sheria” ameanza rasmi safari yake ya kisiasa, na tayari ameongeza joto katika mojawapo ya kinyang’anyiro kitakachofuatiliwa zaidi kuelekea uchaguzi wa mwaka 2027.