Makala

Tshisekedi ampigia simu Ruto baada ya Duale kunyima vibali madaktari wa Congo

Na RICHARD MUNGUTI February 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS Felix Tshisekedi wa DR Congo aliwasiliana na Rais William Ruto Jumatatu Feburuari 2, 2026 kutatua mzozo wa madaktari 50 kunyimwa vibali na leseni kufanya kazi humu nchini, Mahakama Kuu ya Milimani Nairobi iliambiwa.

Jaji Roselyn Aburili alifahamishwa na wakili Danstan Omari kwamba Rais Tshisekedi alimpigia Rais Ruto simu na kuafikiana mzozo huo utasuluhishwa mara moja.

Bw Omari aliomba kesi aliyoishtaki serikali ya Kenya kuwanyima madaktari hao vyeti vya kufanya kazi nchini iahirishwe kwa siku 14.

“Hivi sasa nimeelezwa Rais Tshisekedi amewasiliana na Rais Ruto kusuluhisha suala hili la madaktari kunyimwa leseni na vibali vya kufanya kazi nchini,” Bw Omari alimweleza Jaji Aburili saa nne asubuhi kesi hiyo ilipokuwa inasikizwa.

Bw Omari alimweleza Jaji Aburili kwamba suala hili la madaktari wa Congo kunyimwa leseni limezua mtafaruku wa kidiplomasia kati ya nchi hizi mbili.

Kabla ya Rais Tshisekedi kumpigia simu Rais Ruto, wakili wa serikali Wanjohi Munene na Bw Omari walikuwa wameeleza korti mashauri ya kusuluhisha mzozo huo yameanza.

Bw Omari alifichua mnamo Ijumaa Januari 30, 2026 maafisa wakuu wa Serikali hizi mbili walianza mashauri katika hoteli ya kifahari ya Safari Park kuhusu mzozo huo.

“Naomba hii kesi iahirishwe kwa siku 14 kuyapa mataifa haya mawili fursa ya kuafikiana,” Bw Omari aliiomba korti.

Madaktari hao 50 waliishtaki Wizara ya Afya na Waziri wa Afya Aden Duale kwa kuamuru Baraza la Kitaifa ya Madaktari (KMPDC) lisiwape madaktari wa Congo vibali vya kuhudumu nchini.

Pia idara ya uhamiaji iliwanyima vibali vya kufanyakazi nchini.

Madaktari hao walimshtaki Bw Duale, Wizara ya Afya, Wizara ya Mashauri ya Nchi za Kigeni, KMPDC na Ubalozi wa DR Congo nchini wakidai haki zao zimekandamizwa.

Mahakama iliombwa na Bw Omari ifutulie mbali uamuzi wa Bw Duale na Wizara ya Afya akisema DR Congo ni mwanachama wa Jumuia ya Afrika Mashariki na wanachama wake wanaweza kufanya kazi popote.

Jaji Aburili alimwuliza Bw Munene ikiwa madaktari wa Kenya wanafanya kazi ng’ambo.

“Je madaktari wa Kenya na wauguzi hufanyakazi ng’ambo?” Jaji Aburili alimwuliza Bw Munene.

“Ndio,” Bw Munene alijibu.

Jaji huyo aliendelea kumtaka Bw Munene aeleze jinsi Kenya itakavyofanya ikiwa wataalam wetu watafurushwa kule wanakofanya kazi.

Jaji huyo aliwataka wahusika katika mashauri hayo wayakamilishe katika muda wa siku 90 kwa mujibu wa Kifungu nambari 159 cha Katiba ya nchi hii.

Madaktari hao 50 wa DR Congo wamekuwa wakitoa huduma za matibabu humu nchini kwa zaidi ya miaka 10.

Wamekuwa wakihudumu katika hospitali za kidini na kibinafsi.

Bw Duale alikuwa ameiamuru KMPDC iwaajiri madaktari wa humu nchini kutoa huduma ambazo madaktari hao wa DR Congo huzitoa. Kesi hiyo itatajwa baada ya  siku 14.