Iran yakubali kuongea na Amerika, kwa masharti
TEHRAN, IRAN
RAIS wa Iran Masoud Pezeshkian, amesema wamekubali kujadiliana na Amerika baada ya kushawishiwa na nchi jirani kufanya hivyo.
Kupitia taarifa yake kwenye mtandao wa X, Pezeshkian alisema kuwa amemwaamrisha Waziri wa Masuala ya Nje, Abbas Araghchi ahusike na mazungumzo hayo mradi tu kuwe na mazingira faafu.
Pezeshkian hata hivyo alisema mazungumzo hayo hayafai kushirikisha vitisho kutoka kwa Amerika ama malengo yao kupewa kipaumbele.
Haya yanajiri baada ya Kiongozi wa Kidini Ayatollah Khamenei kuonya kuwa uvamizi wowote dhidi ya Iran kutoka kwa Amerika utasababisha vita vikali.
Rais wa Amerika, Donald Trump alikuwa ametishia kuvamia Iran kutokana na kustawisha kiwanda chake cha kinuklia na pia kuwaandama waandamanaji.
“Mazungumzo hayo yanafanyika chini ya mwongozo wa sheria zetu na maslahi ya nchi yetu,” akaongeza Pezeshkian.
Kwa mujibu wa vyombo vya habari Amerika, mazungumzo hayo yataandaliwa Istanbul mnamo Ijumaa.
“Kama tunaweza kufanya jambo basi hilo litakuwa lakini mambo yasipotengenezwa, mabaya yatatokea,” akasema Rais Trump mnamo Jumatatu.
Mwaka jana Amerika ilivamia vituo vya kinuklia baada ya Israeli pia kulenga vituo hivyo na wanasayansi wa Iran.
Awali, Trump alikuwa amedai kuwa meli za kivita na ndege za Amerika pamoja na wanajeshi walikuwa tayari kushambulia Iran iwapo ingeendelea kuwaua waandamanaji.
Serikali ya Iran imekuwa ikisema watu 3,117 waliuawa wakati wa maandamano hayo ingawa wanaharakati na makundi ya haki yanasema idadi hiyo huenda ikawa ya juu zaidi.
Shirika la Kutetea Haki za Kibinadamu ambalo lina mizizi au makao yake Amerika lilisema kuwa limethibitisha vifo vya waandamanaji 6,430, watoto 152 na watu 214 ambao wanahusishwa na serikali.
Bado shirika hilo linachunguza visa 11,280 vya dhuluma dhidi ya waandamanaji.
Nalo shirika la kutetea haki za kibinadamu la IHR ambalo lina makao yake Norway, limesema kuwa uchunguzi na utathmini wake unaonyesha idadi ya waliouawa na serikali ya Iran ni zaidi ya watu 25,000.
Maandamano Iran yalisababishwa na raia kuchoshwa na kupanda kwa bei ya bidhaa jambo lililofanya gharama ya maisha kupanda sana.
Hata hivyo, yalichukua mwelekeo wa kisiasa wengi wakimsukumu Ayatollah Khamenein ajiuzulu.
Maafisa wa Iran nao wamemwaambia Khamenei kuwa ghadhabu za umma zilitokea wakati wa maandamano kwani wengi walikuwa wakisema kuwa hawamtaki tenaki tena.