Msukumo utafiti utengewe Sh300 bilioni kwa mwaka, ikiwemo kilimo
WATAFITI na Wanasayansi kutoka sekta muhimu kote nchini wanaitaka serikali ya kitaifa kutenga angalau asilimia 2 ya Pato la Taifa (GDP) kila mwaka kwa ajili ya utafiti, ubunifu na maendeleo.
Kupitia kwa National Research Fund (NRF), taasisi ya kiserikali iliyopewa jukumu kufadhili shughuli za utafiti nchini, wataalamu kutoka vyuo vikuu, afya, kilimo, elimu, mabadiliko ya tabianchi, mazingira, uhandisi, sera za umma, miongoni mwa wengine, wanasema kiwango hicho kitawezesha serikali kukabiliana na changamoto kubwa zinazokabili taifa.
Kwa sasa, serikali inatenga asilimia 0.8 ya bajeti ya kitaifa kwa utafiti, kiasi ambacho watafiti wanalalamikia ni kidogo mno kusaidia kikamilifu kutafuta suluhu katika sekta kama afya, elimu, mabadiliko ya tabianchi na kilimo.
Wakizungumza wakati wa mkutano wa kitaifa wa Kenya Research Financing and Capacity Strengthening Masterplan (2026–2036) uliofanyika Nairobi, Mkurugenzi Mkuu wa NRF Prof Dickson Andala alisisitiza umuhimu wa kuongeza uwekezaji katika sekta ya utafiti.

Kwa sasa NRF inasimamia karibu Sh120 bilioni, lakini Prof Andala alisema lengo ni kuongeza kiasi hicho hadi angalau Sh300 bilioni kila mwaka ili kukidhi mahitaji ya kitaifa ya utafiti.
Gapu ya Sh180 bilioni iliyopo, alisema, inalemaza shughuli za utafiti nchini na inahitaji kushughulikiwa haraka.
Kwenye sekta ya kilimo, kwa mfano, alisema athari za mabadiliko ya tabianchi zitaangaziwa kikamilifu endapo utafiti utapata mgao wa kutosha.
“Utafiti unaofadhiliwa ipasavyo, hakuna kikomo cha mafanikio,” Prof Andala alibainisha.
Pendekezo la kutenga asilimia 2 ya GDP ni sehemu ya rasimu ya Mpango Mkuu uliotayarishwa na kamati ya ushauri wa kiufundi ya NRF kwa ushirikiano na ISAAA AfriCenter, na Research and Innovation Systems for Africa (RISA) Fund of the United Kingdom’s Foreign, Commonwealth and Development Office (FCDO).

Utafiti nchini Kenya hufanyika hasa katika taasisi za umma na binafsi, huku vyuo vikuu vikiongoza.
Mpango huo, unaotarajiwa kuzinduliwa mwaka ujao, 2026, unaeleza mkakati wa kukusanya rasilimali kutoka serikalini, sekta ya kibinafsi na washirika wa maendeleo ili kuimarisha sekta ya utafiti.
Lengo ni kuboresha ushirikiano kati ya taasisi za utafiti, serikali na sekta ya viwanda, na kuhakikisha uvumbuzi wa ndani unafikishwa sokoni.
Katibu Mkuu wa Idara ya Utafiti, Ubunifu na Maendeleo Prof Shaukat Abdulrazak alisema serikali imejitolea kuifanya Kenya kuwa uchumi unaoongozwa na maarifa, huku sayansi, teknolojia na ubunifu vikichochea maendeleo ya kitaifa.

Inakadiriwa Kenya hupoteza kati ya asilimia 30 hadi 40 ya mazao ya kilimo msimu wa mavuno, kwa sababu ya ukosefu wa miundomsingi bora.
Kando na sekta ya kilimo, afisa huyo anasema afya, elimu na sekta zingine muhimu kwa taifa pia zitanufauka pakubwa, endapo kiwango kinacholengwa kitatimia.