Wanasiasa maarufu wa eneo la mlima wagomea UDA
ZOEZI la kusajili wawaniaji katika uchaguzi wa 2027 linaloendelea la chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA) limeonyesha kuporomoka kwa mvuto wa chama hicho katika eneo lenye idadi kubwa ya wapiga kura la Mlima Kenya.
Takwimu za chama zinaonyesha kuwa, vigogo wa kisiasa katika eneo hilo wanaonekana kukiepuka chama kilichomwezesha Rais William Ruto kuingia madarakani mnamo 2022.
Katika baadhi ya kaunti, kiti cha ugavana hakikuvutia hata mwanasiasa mmoja wa kuwania dhidi ya magavana walioko madarakani waliochaguliwa kwa tiketi ya UDA.
Hata hivyo, UDA bado kina nguvu katika eneo la Bonde la Ufa kulingana na idadi ya wawaniaji waliojitokeza kujisajili, huku chama hicho kikijaribu pia kupenya katika maeneo ya Magharibi, Pwani na Nyanza.
Aidha, wanasiasa wengi zaidi kutoka ngome za jadi za ODM wanamezea mate tiketi ya UDA ikilinganishwa na ilivyokuwa uchaguzi wa 2022.
Naibu Rais Kithure Kindiki alifafanua kuwa, si lazima kwa viongozi waliochaguliwa kujisajili kama wawaniaji kwa sasa, akisema bado kuna fursa ya kuvutia wanasiasa zaidi kabla ya uchaguzi wa 2027.
“Si lazima magavana, maseneta, wabunge au madiwani walio madarakani kwa tiketi ya UDA wajisajili kwa sasa,” alisema Profesa Kindiki.
“Zoezi la usajili wa wawaniaji ni endelevu hadi kufikia muda wa kisheria wa siku 90 kabla ya tarehe ya uchaguzi.”
Huku baadhi ya kaunti za Bonde la Ufa zikirekodi hadi wagombea 16 wa ugavana, wanasiasa wa Mlima Kenya wanaonekana kuchukua mkakati wa kusubiri na kuona kabla ya kuamua ni chama kipi watatumia kuwania nyadhifa.
Kwa mfano, Baringo imeandikisha wagombea 16 wa ugavana, sita wa seneti, 30 wa mwakilishi wa wanawake, 84 wa ubunge na 479 wa MCA.
Elgeyo-Marakwet ina wagombea 10 wa ugavana, 15 wa seneti, 10 wa mwakilishi wa wanawake, 43 wa ubunge na 278 wa MCA. Kericho imeandikisha wagombea 13 wa ugavana, 11 wa seneti, 17 wa mwakilishi wa wanawake, 71 wa ubunge na 478 wa MCA.
Nandi ina wagombea 10 wa ugavana, 15 wa seneti, 21 wa mwakilishi wa wanawake, 104 wa ubunge na 478 wa MCA.
Bomet ina wagombea watatu wa ugavana, tisa wa seneti, 17 wa mwakilishi wa wanawake, 55 wa ubunge na 366 wa MCA.
Lakini katika Mlima Kenya, hakuna mgombea hata mmoja aliyejitokeza kuwania ugavana katika kaunti za Embu, Murang’a, Laikipia na Nyandarua.
Nyeri, Kirinyaga na Meru zimevutia mgombea mmoja kila moja.
Nakuru na Kiambu zimevutia wagombea watatu kila moja, huku Nakuru ikiwa na mchanganyiko wa jamii mbalimbali.
Takwimu hizo zinamaanisha kuwa, kwa sasa UDA haina mpinzani wa kumpinga Gavana Cecily Mbarire wa Embu, ambaye pia ni mwenyekiti wa kitaifa wa chama na anatarajiwa kutetea muhula wa pili.
Katika kinyang’anyiro cha useneta, tiketi hiyo imevutia wagombea 10, mwakilishi wa wanawake watano, wabunge 13 na MCAs 103. Katika kaunti ya Kiambu, Mbunge wa Thika Town Alice Ng’ang’a ni miongoni mwa wawaniaji watatu wanaotaka kumpinga Gavana Kimani Wamatangi.
Wengine ni Kimani Waceke na Robert Ndirangu.
Gavana Wamatangi hajajitokeza katika orodha ya wawaniaji, ingawa viongozi walio madarakani hawakulazimika kujisajili.
Wengine waliojisajili walifanya hivyo kama ishara ya kujitolea kwa tiketi ya chama.
Gavana Wamatangi pia hakuhudhuria mkutano wa Baraza Kuu la Kitaifa la chama uliofanyika Ikulu wiki iliyopita. Kaunti hiyo ina wagombea tisa wa seneti, sita wa mwakilishi wa wanawake, 31 wa ubunge na 469 wa MCA.
Aliyekuwa Waziri Moses Kuria pia ameomba kuwania kiti cha ubunge Gatundu Kusini.
Katika kaunti ya Kirinyaga, Mbunge wa Kirinyaga ya Kati Joseph Gitari anataka kumrithi Gavana Anne Waiguru anayehudumu muhula wake wa mwisho.
Kaunti hiyo ina wagombea wanne wa seneti, wanne wa mwakilishi wa wanawake, tisa wa ubunge na 95 wa MCA. Kwa jumla, wagombea 12,353 wamejisajili kuwania kwa tiketi ya UDA.
Hii inajumuisha 149 wa ugavana, 279 wa seneti, 323 wa mwakilishi wa wanawake, 1,372 wa ubunge na 10,230 wa MCA.