Kega akimbia kwa Gachagua baada ya Jubilee kumponyoka
ALIYEKUWA Mbunge wa Kieni, Kanini Kega, amejiunga na chama cha aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, Democratic for the Citizens Party (DCP).
Kanini, ambaye ni mwanachama wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) amehamia DCP akitoka chama cha Jubilee ambacho alijaribu kukinyakua kutoka Rais mstaafu Uhuru Kenyatta.
Kupitia mitandao ya kijamii, Gachagua alimkaribisha Kanini katika chama cha DCP, akikitaja kama nyumba ya viongozi wenye mtazamo wa kimaendeleo wanaotamani uongozi wa siku zijazo.
“Karibu nyumbani Mheshimiwa @kaninikega1, @DCP_Democracy ni makao ya viongozi wanaotamani kuongoza siku za baadaye,” alisema Gachagua.
Kanini alichaguliwa kuwa Mbunge wa Kieni mwaka 2017 kwa tiketi ya Jubilee, na mwaka 2022 akateuliwa na chama hicho kuwa mwanachama wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA).
Baada ya kujiunga na Bunge la Afrika Mashariki, Kanini alijikuta katikati ya mgogoro wa ndani ya chama cha Jubilee ulioshuhudia makundi mawili, moja likiongozwa naye pamoja na Mbunge mteule Sabina Chege, na jingine likiongozwa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Jubilee, Jeremiah Kioni.
Kanini na mrengo wake walidai akiwa Rais mstaafu, Kenyatta hafai kuwa kiongozi wa chama, dai ambalo rais huyo wa nne wa Kenya na kundi lake walikataa na kupigana kortini hadi wakatangazwa viongozi halali wa Jubilee.
Baadaye Kanini alibadilisha mwelekeo wake wa kisiasa na kumuunga mkono Gachagua, na ameonekana kuwa mmoja wa watetezi wakuu wa kiongozi huyo wa DCP.
Kuhama kwake kunajiri wakati ambapo wanasiasa mbalimbali wanajiandaa kugombea nyadhifa mbalimbali katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Agosti 2027.
Wanasiasa kutoka Muungano wa Upinzani na muungano tawala wa Kenya Kwanza wameonekana kujipanga kwa lengo la kuimarisha uungwaji mkono kuelekea uchaguzi huo mkuu.