Hakuna Mkenya atakayeaga dunia kwa njaa – Kindiki
NAIBU wa Rais Prof Kithure Kindiki amesema kuwa serikali itahakikisha hakuna Mkenya anayeaga dunia kutokana na njaa kwa sababu ya ukame unaoendelea kushuhudiwa katika baadhi ya maeneo nchini.
Jana, serikali ilitoa Sh4 bilioni za kununua vyakula na bidhaa nyingine za kusambaziwa wakazi wa maeneo yaliyoathiriwa na kiangazi.
Prof Kindiki alifichua kuwa juhudi zimeanza kufanywa za kuwafikia Wakenya ambao wameathirika na baa hilo la njaa.
“Wakenya milioni 3.3 katika kaunti 23 wanahitaji chakula kwa dharura na kaunti nne ziko katika hali mbaya zaidi,” akasema Prof Kindiki baada ya kuandaa mkutano wa kuweka mikakati ya kupambana na ukame na njaa afisini mwake jijini Nairobi.
Kaunti 10 ambazo zimeathirika kwa kiwango kikubwa ni Mandera, Wajir, Garissa, Marsabit, Tana River, Turkana, Kwale, Samburu na Kilifi.
Kaunti nne ambazo ziko katika hali mbaya zaidi ni Mandera, Wajir, Kwale na Kilifi.
Prof Kindiki alisema serikali ilitoa Sh6 bilioni kati ya Desemba 2025 na Januari 2026 kununua vyakula na bidhaa nyingine za kuwagawia wakazi walioathiriwa.