Siasa

Wakili amshtaki Ruto kuhusu mikutano ya UDA kufanyika Ikulu

Na SAM KIPLAGAT February 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAKILI Jijini Nairobi amewasilisha kesi kortini kumzuia Rais William Ruto na chama chake cha UDA kushiriki mikutano ya kisiasa katika Ikulu au ikulu ndogo.

Bw Lempaa Soyinka anasema kwenye kesi iliyowasilishwa katika Mahakama Kuu kwamba matumizi ya ikulu na UDA kwa mikutano ya kisiasa, makundi ya kisiasa, warsha za wagombeaji na shughuli za mipangilio ya chama hicho ni sawa na manufaa yasiyo ya kifedha na ufadhili ambao haujatangazwa usiojumuishwa chini ya kipengee cha 14 cha Sheria ya Vyama vya Kisiasa.

Ameitaka mahakama kuingilia kati kwa dharura na kutoa amri ya kuzuia matumizi ya fedha za umma, rasilimali, wafanyakazi, walinzi, usafirishaji au vifaa kwa shughuli za kisiasa ndani ya Ikulu au ikulu ndogo nyinginezo.

“Matumizi yanayoendelea ya ikulu kwa shughuli za chama cha kisiasa ni ukiukaji wa sheria na yanageuza kuwa kawaida kutumia vibaya rasilimali za umma na kuharibu kabisa utawala wa kikatiba na imani ya umma,” alisema.

Wakili huyo alihoji kuwa ikulu, kama taasisi inayolindwa kikatiba na inayofadhiliwa kupitia rasilimali za umma, inayofanyiwa kazi na maafisa wa umma na kustawisha rasilimali za umma, ni rasilimali ya umma.

Anataka korti itathmini ikiwa matumizi hayo yanajumuisha matumizi ya rasilimali za umma kinyume cha sheria na iwapo kuruhusu UDA kutumia pesa za ikulu kunazidisha uwezo wa kisiasa kwa njia isiyo ya haki kinyume cha demokrasia ya katiba.

Wakili huyo anataka korti ikomeshe vyama vyote vya kisiasa kuandaa mikutano, makundi ya kisiasa, warsha au shughuli za kisiasa katika Ikulu au Ikulu ndogo.

Alitaja mikutano kadhaa ukiwemo wa Agosti 15, 2025, wakati Rais Ruto aliwakaribisha viongozi wanasiasa wa jamii ya Gusii katika ikulu, Nairobi na mkutano mwingine Agosti 27, alipokutana na viongozi wa mashinani Kiambu, na viongozi kutoka Ukambani, Oktoba 10.

Juni 5, Rais Ruto aliwapokea Ikuluni wajumbe kutoka Vihiga, Kakamega, Busia, Bungoma, Trans Nzoia na Siaya na majuzi Januari 26, 2026, alipoongoza mkutano wa baraza kuu la UDA kabla ya kuandaa warsha ya kwanza ya wagombea wa UDA, Februari 4.

“Matukio haya hayakuwa hafla za kitaifa, maadhimisho au mikutano ya serikali tawala, bali shughuli za kisiasa zinazohusu maafisa wa chama, wagombea na viongozi waliochaguliwa waliojitokeza katika nafasi yao ya kisiasa,” alisema.

Bw Suiyanka alisema matumizi ya ikulu kwa shughuli za kisiasa za chama yanakiuka Kifungu 10 cha katiba.