Wanawake wanavyofanikisha kilimohai, endelevu
MKULIMA Beatrice Wangare Kamau, kutoka Molo, Kaunti ya Nakuru, amekuwa akikuza nafaka na mboga kwa zaidi ya miaka 20.
Hata hivyo, kwa muda mrefu athari za mabadiliko ya tabianchi zimeendelea kutatiza jitihada zake za kilimo.
Hulima mahindi, maharagwe, minji, kabichi, nyanya, vitunguu, karoti, pamoja na mboga kama sukuma wiki na spinachi.
Athari za tabianchi zinazokumba Kenya na Bara la Afrika zimepunguza kwa kiasi kikubwa mavuno yake, hali iliyomlazimu kubadili mbinu zake za zaraa.

Changamoto hizo zilichangiwa zaidi na utegemezi wa muda mrefu wa fatalaiza yenye kemikali, ilimuradi aweze kuongeza mazao mara dufu.
Wangare, hata hivyo, anakiri kwamba mbolea hiyo haisaidii wakulima tena kama ilivyokuwa hapo awali.
“Afya ya udongo imedhoofika na inaendelea kuharibika, yote haya yakiwa athari za tabianchi,” anasema.
Miaka michache iliyopita, Wangare alifanya maamuzi ya kuhamia kilimohai na endelevu na kuacha matumizi ya pembejeo zenye kemikali.

Aidha, amekumbatia agroekolojia (agroecology), mfumo jumuishi wa kilimo unaozingatia mazingira na kuyadumisha, na anasema umebadilisha pakubwa uzalishaji wake.
Mifumo ya agroekolojia aliyokumbatia ni pamoja na mzunguko wa upanzi wa mimea (crop rotation), kilimo mseto (mixed farming), matumizi ya mbolea ya mifugo, kilimo hifadhi, kilimo-misitu, udhibiti wa wadudu na magonjwa kwa kutumia dawa asilia za kujiundia, na umwagiliaji mimea na mashamba maji kwa kutumia mifereji (irrigation).
Isitoshe, ameanzisha kilimo cha bustani ambapo hukuza mseto wa mboga.
“Shamba langu lina mifugo; ng’ombe, mbuzi, kondoo na kuku. Natumia samadi kama mbolea asilia kupanda mimea badala ya fatalaiza ya viwandani,” anaelezea.

Anaongeza, “Mbinu nilizokumbatia zinapunguza pakubwa utegemeaji wa fatalaiza zenye kemikali, na kuimarisha uwezo wa wakulima kukabiliana na athari za tabianchi, wakati huohuo zikilinda mazingira.”
Wangare anakiri kiwango cha mazao kuongeza. “Ekari moja ya mahindi ambayo awali ilikuwa ikizalisha magunia 15 ya kilo 90 sasa inanipa zaidi ya magunia 40,” anasema.
Simulizi yake si tofauti na ya Agnes Mwende kutoka Makueni, anayelima mazao yanayostahimili ukame kama vile mtama, wimbi, ndengu, mahindi, na mboga za kienyeji; managu, terere na kunde.
Agnes, kwenye mahojiano na Akilimali alisema wanafanikisha hilo kupitia kikundi cha Smart Future Bio-Diversification Farming F.S.C.

“Tumeamua kilimo endelevu kupitia mfumo wa agroekolojia ndio suluhu ya uhaba na ukosefu wa chakula,” Agnes anasisitiza.
Kundi hilo, pia huongeza mazao thamani – kupitia uchakataji.
Kwa wanaoongeza thamani bidhaa za kilimo, mifumo ya agroekolojia pia imewafaa pakubwa.
“Uongezaji thamani kando na kumpa mkulima hela, mazao yaliyokuzwa kwa kuzingatia mifumo asilia yanasakwa sana na walaji – wateja,” anaelezea Christina Oforo, mkulima kutoka Tanzania.
Christina ni Mkurugenzi wa Organic Moringa Herbal Products, kampuni inayochakata chakula asilia. “Kwa mfano, mafuta ya moringa yaliyokamwa yana ushindani mkuu sokoni,” anaelezea.

Wangare, Agnes na Christina, wanasema mifumo endelevu waliyokumbatia walisomeshwa na Muungano wa Participatory Ecological Land Use Management (PELUM) – matawi ya Kenya na Tanzania, na Kenya Cereal Enhancement Programme (KCEP), mashirika yanayohamasisha agroekolojia.
Hadithi za aina hiyo, zilikuwa kati ya zilizoibuliwa wakati wa Warsha ya Wanawake Viongozi kwenye Agroekolojia Barani Afrika (AWOLA) 2025 iliyofanyika Nairobi kati ya Desemba 2 na 3.

Ikiwa ni Makala ya Tatu yenye kaulimbiu “Bold Voices: Championing African Women’s Leadership in Food Sovereignty through Land Rights, Agroecological Entrepreneurship, and Territorial Markets”, hafla hiyo inayoandaliwa na PELUM Kenya kila mwaka ilileta pamoja zaidi ya washirika 100 kutoka mataifa mbalimbali Afrika, wakiwemo kina mama kutoka mashinani, wakulima, wanasheria, vijana na wadauhusika wengine wanaohamasisha kilimohai na endelevu.
Monica Nyaga wa PELUM, kwenye mahojiano alisikitika kwamba wanawake licha ya kuchangia zaidi ya asilimia 70 ya nguvukazi ya kilimo, sauti zao hazisikiki vya kutosha.

“Mifumo ya kilimo endelevu, kama agroekolojia ndiyo itasaidia kuangazia changamoto za chakula Kenya na Barani Afrika kwa jumla. Wanawake wanachangia pakubwa kwa uzalishaji wa chakula na sauti zao zinapaswa kuskika,” Monica akasema.
Tangu kuanzishwa 2023, AWOLA imepenyeza mizizi yake Kenya, Zimbabwe, Uganda, Malawi, na Nigeria, na kwenye warsha ya 2025 wanawake 60 walifuzu kwa mafunzo ya agroekolojia.
Kenya, mwaka 2024 ilipitisha Sheria ya Agroekolojia 2024 – 2033.
Kaunti kama Murang’a, Vihiga, Kiambu na Nakuru tayari zimepitisha sheria hiyo kama serikali za ugatuzi.
Zingine zinazoshughulikia ni pamoja na Busia, Kakamega, Laikipia, and West Pokot.

“Agroekolojia si utamaduni wa kizamani; ni mfumo wa kilimo unaoweza kuongeza uzalishaji na kuzuia magonjwa yanayohusiana na lishe kabla hayajatokea. Sokoni tunasema mama mboga, na si baba mboga, jambo linaloashiria nafasi kuu ya wanawake katika mifumo ya chakula.
“Hata hivyo, licha ya mchango wao mkubwa, wengi wao hukosa rasilimali kama vile umiliki wa ardhi kwa sababu ya vikwazo vya kitamaduni. Hili lazima lishughulikiwe,” anahimiza Dkt Susan Chomba, Mkurugenzi wa Chakula, Ardhi na Maji katika taasisi ya World Resources Institute (WRI).
Nchini Kenya, wanaharakati wa agroekolojia wanaitaka serikali kuanzisha mpango wa ruzuku—unaofanana na ruzuku ya mbolea, ili kufanikisha kilimo endelevu.
Mifumo endelevu ya kilimo huimarisha rutuba na afya ya udongo, hivyo kusaidia wakulima kukabiliana na athari za tabianchi.