Mwalimu mstaafu anavyojisitiri kijijini kwa mazao yanayokomaa upesi
KEZIAH Wangui alipostaafu kama mwalimu wa elimu ya watu wazima mwaka wa 2020 baada ya kufanya kazi hiyo kwa zaidi ya miaka 30, aliacha kilimo cha mahindi ambacho alikuwa amekifanya kwa miaka mingi na kuhamia mazao ya muda mfupi katika shamba lake la Turi mjini Elburgon, Kaunti ya Nakuru.
“Uamuzi wangu wa kulima mazao ya muda mfupi ulikuja baada ya kugundua kuwa uzalishaji wangu katika kilimo cha mahindi mwishoni mwa kila msimu ulikuwa unapungua, gharama kubwa ya pembejeo za shambani, kupata mauzo duni huku sekta hiyo ikitawaliwa sana na madalali,” akasema Wangui.
Anaeleza kuwa alianza kwa kupanda mazao ya msimu yaliyonunuliwa upesi sokoni kama vile vitunguu, viazi, brokoli na karoti miongoni mwa mimea mingine.
Kwa mtaji wa Sh2,000 alizokuwa nazo, aliandaa sehemu moja ya shamba lake mnamo 2025 na kutumia Sh400 kwa kununua gramu 100 za mbegu na kukuza za miche ya karoti ambayo alipanda kwenye eneo alilotenga huku akitumia salio la fedha zake kwa kulipa wafanyikazi.
Anaeleza kuwa alichanganya udongo na samadi ya kondoo na kupanda miche kwenye mitaro aliyochimba.
“Kati ya siku 7 hadi 14, miche iliota nami nikainyunyizia dawa ili kuua magugu. Mwezi mmoja baada ya kupanda, nilianza kupalilia na kuendelea kunyunyizia dawa, hasa wakati wa msimu wa baridi kwani mimea huathiriwa na barafu,” anasema Wangui, akiongeza kuwa karoti hukua vizuri zinapopandwa na kukuzwa wakati wa msimu wa mvua.
Hata hivyo, amechimba kisima shambani kama moja ya hatua mbadala zinazomsaidia kuendelea kukuza mazao wakati wa kiangazi.
Wangui anasema karoti hukomaa na kuwa tayari kuvunwa baada ya miezi mitatu,huku akiongeza kuwa ni nadra sana karoti kuathiriwa na wadudu au vidukari.
“Niliziuza katika soko la ndani kwa Sh400 kwa kila mkebe wa kilo 17,” anaeleza.
Anasema kuwa mazao ya muda mfupi yanahitaji uangalifu vyema kwani wakulima hulenga soko zuri.
Kwa kuwa wakulima wengi katika eneo hilo hawakuwa wamekuza aina hiyo kwa wakati huo, mauzo yalikuwa ya kutia moyo na hii ilimvutia na kumfanya apanue shamba lake hadi robo na kupanda karoti zaidi kwa sababu soko lilikuwa na mahitaji makubwa na wateja wengi.
“Mnamo Machi mwaka huu, nilitumia Sh4,000 kwa ajili ya maandalizi ya shamba,kununua miche na upanzi katika eneo jipya ambalo niliongeza. Nilinunua gramu 500 za miche kwa Sh1,700 na kutumia taratibu za upanzi kama vile nilifanya kwenye sehemu yangu ya awali. Nilipanda miche yangu kwenye mitaro na kutumia mbolea asilia kutoka kwa kondoo, kuku na bata,” anasema Wangui, akiongeza kuwa mwaka huu, mvua ilikuwa ya kutosha tofauti na misimu mingine ambapo huwa changamoto.
Anaeleza kwamba tangu alipoanza kulima karoti, hajawahi kukumbana na wadudu au magonjwa yoyote kama inavyotokea kwenye mazao mengine.
Kama njia bora ya uangalifu na usimamizi wa mazao, aliendelea kufuatilia, kupalilia na kutumia dawa za kuua magugu, kulingana na hali ya hewa ili kuhakikisha kwamba mazao na uzalishaji wake unastawi kwa kiwango cha kuridhisha na kukidhi mahitaji ya wateja wake.
Wangui anasema kuwa biashara ya karoti na viazi imestawi katika eneo hilo kufuatia uhaba sokoni wa mazao ya shamba yanayotumiwa sana.
Kwa hivyo, bei zimeongezeka huku ikichangiwa na uhaba wa bidhaa hizi miongoni mwa aina nyingine za muda mfupi zinazotumiwa sana sokoni.
“Kwa sasa, mkebe wa kilo 17 anauza kwa Sh800 kutoka Sh400 katika soko la ndani katika wiki chache zilizopita. Sijaweza kukidhi mahitaji ya wateja wangu ambao hutembelea shamba langu kila siku kununua bidhaa hiyo ambayo ina mahitaji makubwa,” anasema.
Katika miaka mitano ijayo, mpango wake ni kuwekeza na kukuza mazao ya muda mfupi katika eneo kubwa la ekari tano ambalo litaweza kuwaridhisha wateja wake.
Pia, anakusudia kufuga kondoo na kuku kwa wingi ili kuvuna mbolea zaidi na kuitumia shambani na kuongeza uzalishaji wa mazao yake kupitia kilimo hai.
Ili afanikiwe shambani, mkulima hufanya mzunguko wa mazao ili kuzuia kuenea kwa magonjwa na bakteria wanaojificha kwenye udongo, haswa wakati zao fulani la familia moja linapandwa katika eneo moja kwa muda mrefu.
Wataalamu wa lishe wanataja faida za kiafya katika karoti kama zenye lishe nyingi, husaidia katika kuona na kukuza afya ya macho, husaidia katika usimamizi mzuri wa uzito, hudhibiti damu na kusaidia mfumo imara wa kinga.
Pia husaidia katika usagaji chakula, udhibiti wa sukari kwenye damu, afya ya ngozi na moyo miongoni mwa mengine.
Ili kufahamu na kuongeza ujuzi wake wa kilimo, Wangui hutembelea maonyesho ya kilimo, huhudhuria semina, siku za shambani na hufanya utafiti mitandaoni.
Hii imemwezesha kujifunza kuhusu teknolojia mpya za kilimo, kuboresha mifumo yake ya kilimo, magonjwa na udhibiti wa wadudu miongoni mwa mengine.
Vilevile, anataja uwepo wa maafisa wa nyanjani kuwa wachache ama kutokuwepo kabisa na hii ni moja ya changamoto kuu zinazowakabili wakulima wadogo katika eneo hilo.
“Serikali ya kaunti inapaswa kutuma maafisa wa nyanjani kwa wakulima na kuwahamasisha kuhusu teknolojia mbalimbali za kilimo, njia za kupunguza kuenea kwa magonjwa na wadudu na kuhakikisha kwamba uzalishaji wao unafanikiwa,” anasema.
Anaongeza, “Uhaba huu au ukosefu wa maafisa wa kutosha umechangia wakulima wengi kutegemea kazi ya kubahatisha kwa sababu hawawezi kuelezea rasmi kiasi na mavuno kutoka kwa shamba ama eneo fulani linalozalisha kwa kilo au tani.”
Kadhalika, anasema kuwa kaunti inapaswa pia kutafuta masoko bora kwa wakulima na kuwaunga mkono kwa kuwapa matangi ya maji ambayo yangewasaidia kuvuna maji zaidi wakati wa mvua na kuyatumia wakati wa kiangazi ili kuongeza uzalishaji wao.