Lugha, Fasihi na Elimu

Makosa ya kawaida wakati wa kutunga sentensi kwa kutumia ‘nguvu’ na ‘sauti’

Na HELLEN NJAGI June 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MOJAWAPO ya mambo muhimu ya kuzingatia unapotunga sentensi ni maana ya maneno unayotumia.

Ikiwa utakosa kufahamu maana ya neno huenda sentensi utakayotunga ikakosa kuwa sahihi au ikawasilisha ujumbe tofauti na uliotarajia.

Neno nguvu aghalabu hutumiwa visivyofaa katika sentensi. Mtu anapokosa kusikika vyema anapozungumza utasikia akiambiwa “Ongeza nguvu.” Au “sema kwa nguvu.”

Katika kusema tunatumia neno sauti badala ya nguvu.

Neno nguvu humaanisha kuwa na msukumo mkali unaotokana na nishati halina maana ya kutoa mlio.

Neno sauti ndilo lenye maana ya mlio. Kwa hivyo, mtu anapokosa kusikika anapozungumza anafaa kuambiwa, “Ongeza sauti, au Sema kwa sauti. Vilevile anaweza kuambiwa, “Paza sauti”.

Kosa jingine lililozoeleka tunapotunga sentensi zenye maneno nguvu na sauti ni kutumia kiunganishi ‘na’ badala ya ‘kwa’ ya kuonyesha jinsi au namna.

Ni kawaida kupata sentensi kama vile: ‘Walilisukuma gari lililokwama na nguvu’ au ‘Wanafunzi waliimba na sauti’.

Sentensi hizo japo zinaeleweka, zimetumia kiunganisho ‘na’ ambacho kimesababisha uwasilishaji wa maana isiyofaa.

Pia si sahihi. Ni kana kwamba ‘nguvu’ ni mtu anayeweza kusukuma gari. Wanafunzi kuimba na sauti pia inamaanisha wanafunzi walikuwa pamoja na ‘sauti’ walipoimba.

Ili kuonyesha jinsi kitendo kilivyofanyika tunafaa kutumia kwa ya jinsi au namna.

Kwa hivyo tunafaa kusema: Walilisukuma gari lililokwama kwa nguvu. Wanafunzi waliimba kwa sauti. Tuendelee kujifunza maana ya maneno mbalimbali ili kuimarisha mawasiliano.