Kimataifa

Ethiopia yashutumiwa vikali baada ya kubainika imeanzisha kambi ya mafunzo kwa RSF

Na REUTERS February 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

ADDIS ABABA, ETHIOPIA

ETHIOPIA inaendelea kuwa eneo la siri la mafunzo ya kijeshi kwa wapiganaji wa RSF katika taifa jirani la Sudan.

Uwepo wa kambi hiyo sasa unaonyesha kuwa Ethiopia inahusika moja kwa moja na ghasia za kijamii ambazo zinaendelea kati ya wanajeshi wa serikali na wapiganaji wa RSF Sudan.

Duru kadhaa kutoka serikali ya Ethiopia zilisema kuwa kambi hiyo ya kijeshi inadhaminiwa na Mmilki ya Kiarabu.

Nchi hiyo imetoa vifaa vya mazoezi, wanajeshi wakufunzi pamoja na misaada mingine inayohitajika na wapiganaji wa RSF.

UAE imekuwa ikikanusha kuwa inawafadhili wapiganaji wa RSF na pia haijaweka wazi iwapo ni kweli inahusika na uendeshaji wa kambi ya mazoezi ambayo ipo Ethiopia.

Vita vya kijamii Sudan vilianza mnamo 2023 kati ya wanajeshi wa Sudan na RSF kuelekea mchakato wa kukabidhi utawala wa taifa hilo kwa raia.

Vita hivyo vimeendelea huku njaa, ukame na ukabila kati ya changamoto nyingine nazo zikiendelea kushuhudiwa nchini humo.

Kutokana na vita hivyo, wakimbizi wametorokea Misri, Chad, Libya na Sudan Kusini.

Kinachosikitisha ni kuwa serikali na RSF zote zinaungwa mkono na mataifa ya nje na kusababisha vita hivyo kuenea zaidi kiasi kwamba hata mataifa jirani huenda yakashirikishwa.

Kwa mfano, serikali ya Rwanda imekuwa ikishutumiwa kwa kuunga mkono kundi la RFS jambo ambalo serikali hiyo imekuwa ikikana.

Inadaiwa shughuli za mafunzo zilianza kunoga katika kambi hiyo inayopatikana eneo la magharibi la Benishangul-Gumuz karibu na mpaka na Sudan.

Mnamo Januari 6, UAE na Ethiopia zilitoa taarifa ya pamoja ambapo zilitoa wito wa kusitishwa kwa vita Sudan na kusherehekea ushirikiano wao wa kiuchumi.

Abu Dhabi imekuwa mshirika wa karibu wa Ethiopia na utawala wa Waziri Mkuu Abiy Ahmed tangu 2018.

Mataifa haya yamekuwa yakishirikiana kwenye mawanda ya mafunzo ya kijeshi tangu wakati huo.