Ukaguzi wabaini Sh5 bilioni zimekuwa zikimezwa na wanafunzi hewa
HUENDA Wakenya wamekuwa wakipoteza takriban Sh5 bilioni kila mwaka kutokana na takwimu zisizo sahihi za usajili wa wanafunzi shuleni, kulingana na ufichuzi uliotokana na ukaguzi wa kuthibitisha wanafunzi uliotekelezwa na Wizara ya Elimu kote nchini.
Ukaguzi huo, uliofanyika kati ya Septemba na Desemba mwaka jana, unaonyesha kupungua kwa wanafunzi katika shule za msingi kwa asilimia 16.5 na asilimia 2.64 katika shule za upili baada ya wanafunzi ambao hawakuthibitishwa kuondolewa kwenye rekodi rasmi.
Kwa kuwa ufadhili wa serikali hutolewa kwa misingi ya idadi ya wanafunzi, hatua hii ina athari kubwa kwa jinsi fedha za umma zilivyokuwa zikigawanwa miaka iliyopita.
Hata hivyo, haijabainika ni kwa muda gani serikali imekuwa ikitumia takwimu hewa kufadhili mipango ya elimu.
Kwa kutumia viwango vya wastani vya mgao wa serikali, takriban Sh1,420 kwa kila mwanafunzi wa shule ya msingi na Sh22,244 kwa mwanafunzi wa shule ya upili kwa mwaka, idadi mpya ya wanafunzi inaashiria kuwa takriban Sh3.4 bilioni katika shule za msingi na Sh1.9 bilioni katika shule za upili huenda zilikuwa zikilipwa kwa misingi ya takwimu ambazo hazikuweza kuthibitishwa.
Hii inafanya kiwango cha fedha za umma ambazo zilitolewa kwa wanafunzi hewa kwa mwaka kufikia takribani Sh5.3 bilioni.
Kiasi hiki hakijajumuisha mgao wa shule za Sekondari Msingi, pesa za miundomsingi na fedha za Elimu ya Mahitaji Maalum, jambo linaloashiria kuwa hasara halisi huenda ni kubwa zaidi.
Kulingana na ripoti ya ukaguzi, maelfu ya wanafunzi waliondolewa kwenye ufadhili baada ya kushindwa kukidhi masharti, ikiwemo kukosa vyeti vya kuzaliwa, maelezo duni ya mwanafunzi au kutofautiana kwa rekodi za shule.
Ni wanafunzi waliothibitishwa kikamilifu pekee waliobaki kuzingatiwa kwa ufadhili. Aidha, shule 26 zilipatikana kuwa hazifanyi kazi, yaani hazitoi huduma za elimu kwa sasa kutokana na kufungwa, ukosefu wa walimu au miundomsingi duni.
“Ukaguzi na uthibitishaji umeidhinisha shule 53,015 kwa mgao, zikiwa na jumla ya wanafunzi 11,028,861. Ingawa shule nyingi zilizingatia masharti, shule 181 ziliwasilisha data kwa mifumo isiyoidhinishwa, 24 bado hazikuwasilisha, shule 495 zilikuwa na nambari halali za vituo tofauti za Baraza la Kitaifa la Mitihani KNEC.
Kwa sasa, shule 26 zimeorodheshwa kama zisizofanya kazi,” ripoti inasema.
Ripoti hiyo pia inaonyesha kuwa shule 1,841 za msingi na shule 1,661 za Sekondari Msingi hazikuwasilisha data yoyote, huku shule 38 za Elimu ya Mahitaji Maalum zikikokosa wanafunzi, hali inayozua maswali kuhusu usimamizi na uwajibikaji katika sekta ya elimu.
Matokeo haya yanathibitisha wasiwasi wa muda mrefu ambao umekuwa ukiibuliwa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kuhusu kuwepo kwa “wanafunzi hewa” na dosari katika takwimu za usajili, ambazo huweka sekta ya elimu katika hatari ya matumizi mabaya ya fedha za umma.
Mnamo Julai 2025, ripoti maalumu ya ukaguzi ilifichua kuwa walipa ushuru walipoteza zaidi ya Sh3.7 bilioni kutokana na wanafunzi hewa na shule zisizokuwepo, kufuatia dosari kubwa katika Mfumo wa Kitaifa wa Usimamizi wa Taarifa za Elimu (NEMIS).
Ukaguzi huo, ulioidhinishwa na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Umma (PAC), uligundua kuwa shule kadhaa zilipokea fedha kupita idadi halisi ya wanafunzi.
Ukaguzi huo pia ulifichua udhaifu wa kitaasisi katika mfumo wa NEMIS. Wachambuzi wanasema ukosefu wa ukaguzi wa mara kwa mara uliwezesha takwimu zisizo sahihi kudumu kwa miaka mingi bila kubainika.
Ripoti ya ukaguzi ilipendekeza wizara ianzishe mfumo wa kisasa wa taarifa za elimu ili kudhibiti kikamilifu usajili na ufadhili wa elimu nchini.