Jamvi La Siasa

Magavana wasusia kamati ya Seneti wakitaja maseneta wanne ‘wakali wa hongo’

Na CECIL ODONGO February 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

BARAZA la Magavana Nchini (COG) limetangaza kuwa magavana hawatafika mbele ya Kamati ya Uhasibu kwenye Bunge la Seneti wakidai maseneta wanne kwenye kamati hiyo wamekuwa wakiwaitisha hongo, kuwatishia na kuwahangaisha.

COG imesema maseneta hao wana mazoea ya kutaka hongo kila mara magavana wanapotakiwa kufika mbele ya Bunge la Seneti kujibu maswali kuhusu matumizi ya pesa za ugatuzi kwenye kaunti.

“Tumechoshwa na kuitishwa hongo, kuhangaishwa na kutishiwa tunapofika mbele ya Kamati ya Seneti kuhusu uhasibu. Maseneta hao wanne wamekuwa wakibobea katika kushiriki tabia hizi,” ikasema taarifa hiyo iliyowataja wanne hao hao na kuwamulika.

Magavana hao walisisitiza kuwa hawatafika mbele ya kamati hiyo ya uhasibu hadi masuala ambayo wameyaibua yatatuliwe kupitia mashauriano na uongozi wa Seneti.

“Malalamishi yetu lazima yaangaziwe na yashughulikiwe kuhusu suala hilo,” ikasema taarifa hiyo iliyotiwa saini na magavana 40 kati ya wote 47.

Kamati hiyo hasa hupiga msasa ripoti za matumizi ya pesa za ugatuzi katika kila mwaka wa kifedha.

Magavana wamekuwa wakifika kujibu masuala wakati mwingine majibizano yakizuka kati yao na maseneta kuhusu ubadhirifu wa kifedha za umma.

“Magavana wanataka maseneta hao wanne waondolewe kwenye kamati hiyo kuhakikisha uwazi, maadili na haki katika mchakato wa kuangazia matumizi ya fedha za kaunti,” ikaongeza taarifa hiyo huku wakisisitiza viongozi hao wahamishwe hadi kamati nyingine.

Kwenye barua hiyo kwa Spika wa Seneti Amason Kingi, wametaka kuwe na mazungumzo kuhusu suala hilo ili wakingwe dhidi ya kuhangaishwa, kutishwa, kuitishiwa hongo na kuadhibiwa kisiasa.

“Tunaunga mkono uwazi kwenye matumizi ya pesa za umma lakini upigaji msasa lazima uzingatie sheria wala usitumiwe vibaya dhidi ya magavana,” wakasema.

Wengi wanasubiri kuona mkondo ambao uhasama huu utachukua wakati ambapo maseneta wamekuwa wakiwalaumu magavana kwa ufisadi.

Baadhi ya maseneta pia wanasaka ugavana 2027 na kumekuwa na madai kuwa wanawahangaisha wanaohudumu kwa sasa ili kupata umaarufu wa kisiasa.