Siasa

Binti ya mwanzilishi wa ODM Winnie Odinga akaidi mjombake, aunga mkono Sifuna

Na BENSON MATHEKA February 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

BINTI ya mwanzilishi wa chama cha ODM Raila Odinga, Winnie Odinga, ambaye ni Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA), ameonekana kumpinga mjomba wake na kiongozi wa ODM, Dkt Oburu Oginga na kumuunga mkono Katibu Mkuu aliyeng’olewa, Seneta Edwin Sifuna.

Winnie aliungana na Bw Sifuna na waasi wengine wa ODM katika mkutano na wanahabari jijini Nairobi jana, siku moja baada ya Oburu kuongoza kikao cha Baraza Kuu la Kitaifa la ODM ambalo lilimtimua Sifuna katika wadhifa wake.

Kabla ya mkutano wa jana ambao Sifuna alipuuza kutimuliwa kwake, Winnie alichapisha ujumbe katika mitandao ya kijamii, akielezea kutoridhishwa kwake na uamuzi wa kikao kilichoongozwa na Oburu wa kumvua seneta huyo wadhifa wake.

“Mambo si shwari,” aliandika katika bango lililokuwa na rangi ya chungwa ya chama hicho. Winnie amekuwa mkosoaji mkubwa wa mwelekeo wa chama hicho tangu kifo cha baba yake Oktoba 2025.

Katika mahojiano Januari 27, 2026, alidai mchakato wa mabadiliko ya uongozi ndani ya ODM haukuwa wa kikatiba na ulifanywa kwa siri.

Alishutumu kikundi kidogo cha viongozi kwa kupuuza wanachama na kufanya maamuzi bila kuwahusisha.