Mikono ya Uhuru, Ruto katika mzozo wa ODM
MGAWANYIKO ndani ya Chama cha Orange Democratic Movement (ODM) umechukua mkondo mpya huku tuhuma nzito zikielekezwa kwa Rais William Ruto na Rais mstaafu Uhuru Kenyatta kwa kile kinachodaiwa kuwa kuingilia masuala ya ndani ya chama hicho.
Mvutano huo umeongezeka kufuatia kuondolewa kwa Katibu Mkuu Edwin Sifuna na Baraza Kuu la Kitaifa (NEC), hatua iliyosababisha makundi mawili kuvutana hadharani kuhusu mustakabali wa chama kuelekea uchaguzi wa 2027.
Mwenyekiti wa ODM Gladys Wanga anadai kuwa Uhuru hafurahii chama hicho kuendeleza ushirikiano wake na UDA.
“Tuko pale ambapo kiongozi wa chama chetu alituacha na tunajua wanaosuka ajenda ya kutugawanya. Mmoja wao ni Rais mstaafu Uhuru Kenyatta,” Wanga alisema akioenekana kudai kuwa Uhuru anaunga mrengo wa waasi wa ODM wanaoongozwa na Sifuna. Kulingana naye, baadhi ya viongozi nje ya chama wanajaribu kusukuma ajenda ambayo inatishia umoja wa ODM, akitaja Uhuru kama mmoja wao.
Tunajua Uhuru Kenyatta angependa ODM isifanye kazi na upande huu na badala yake ijiunge na kundi la Wamunyoro,” alisema Wanga, akirejelea muungano wa kisiasa unaohusishwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua.
Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa, Junet Mohamed, amemshutumu Uhuru Kenyatta akidai ndiye chanzo cha migogoro ndani ya ODM. “Tatizo letu si Ruto. Tatizo letu ni Uhuru Kenyatta. Aache chama chetu na ashughulikie Jubilee na mradi wake,” alisema Junet akiwa Lamu.
Hata hivyo, Gavana wa Siaya James Orengo alimlaumu Rais Ruto moja kwa moja kwa kile alichokiita juhudi za kudhoofisha vyama vya kisiasa. “Niliwahi kumwambia Rais Ruto asiue vyama vya siasa. Tatizo katika ODM ni Rais William Ruto,” alisema Orengo.
Seneta wa Vihiga na Naibu Kiongozi wa ODM, Godfrey Osotsi, aliibua madai mazito akisema mashauriano muhimu kabla ya mkutano wa NEC yalifanyika Ikulu.
“Nilishangaa sana kwamba badala ya kushauriana na wadau wa chama, walienda Ikulu kushauriana na William Ruto. Ndio maana sisi wawili hatukuhudhuria mkutano wa Mombasa,” alisema Osotsi.
Kauli hiyo imeongeza uzito wa madai kwamba maamuzi ya kumwondoa Sifuna hayakuwa ya ndani pekee bali yalihusisha ushawishi wa nje.
Aidha, wachambuzi wanatafsiri matamshi ya awali ya Rais Ruto kama dalili ya mkakati mpana wa kisiasa.
Mwaka jana, Ruto alinukuliwa akisema hatakubali ODM kubaki katika upinzani bali itakuwa sehemu ya mpangilio mpana wa kitaifa wa kuunda serikali. Kauli hiyo ilichukuliwa na baadhi kama ishara kwamba ataingilia masuala ya ndani ya ODM.
Mchambuzi wa siasa Francis Kimani anasema mvutano huo unaonyesha mapambano ya urithi baada ya Raila.
“ODM ilikuwa imejengwa sana kwa haiba ya Raila. Baada ya kuondoka kwake, makundi yanatafuta mwelekeo. Tuhuma dhidi ya Ruto na Uhuru zinaonyesha vita vya ushawishi wa kisiasa,” asema.
Kwa upande wake, Profesa Gitile Naituli anasema lawama kwa Uhuru na Ruto ni sehemu ya siasa za kujihami.
“Vyama vinapokosa mwelekeo wa ndani, mara nyingi hutafuta adui wa nje. Ukweli ni kwamba ODM inapaswa kuamua kama ni chama cha upinzani au mshirika wa serikali,” anasema.
Kimani anaonya kuwa mgawanyiko huo unaweza kukigharimu chama kisiasa.
“Iwapo ODM haitasimamia mazungumzo ya ndani na kujenga mwafaka, inaweza kupoteza umaarufu wake hasa ngome zake za jadi na ndivyo Ruto anataka. Migogoro ya wazi hadharani huathiri imani ya wanachama,” asema.
Kuondolewa kwa Sifuna na kuzuiwa kwa hatua hiyo na Mahakama Kuu kumeongeza joto la kisiasa ndani ya chama.
Wakati kundi moja likiunga mkono ushirikiano na Ruto, jingine linataka ODM isimamishe mgombea wake wa urais 2027.
Kwa sasa, macho yote yanaelekezwa kwa vikao vijavyo vya chama ambavyo vitaamua iwapo ODM itaendelea kushikamana au mgawanyiko huo utaendelea kupanuka.
“Swali kuu linalosalia ni iwapo madai ya mkono wa Ruto na Uhuru ni ukweli wa kisiasa au ni kivuli cha mapambano ya ndani ya chama kinachojaribu kujitafuta baada ya enzi ya Raila.
Akizungumza katika mazishi ya aliyekuwa mbunge wa Lugari Cyrus Jirongo, Uhuru alikanusha madai kuwa anajaribu kukigawa ODM akisema anaheshimu chama hicho na wanachama wake na hana nia ya kuingilia masuala yake ya ndani.
“Mtu anaposhindwa kukubalika anapoenda, anaanza kutafuta mtu wa kumlaumu, akidai watu hawamsikii kwa sababu ya fulani au fulani. Ondoeni mawazo hayo, nendeni mkazungumze na wananchi moja kwa moja. Undeni chama chenu, jengeni sera zenu badala ya kuzunguka mkitoa matamshi ya kipuuzi yasiyoipeleka nchi popote,” alisema Uhuru.