Dereva aliyefutwa kazi sababu ya penzi kulipwa Sh800,000
SHIRIKA lisilo la kiserikali limeagizwa na korti kumlipa aliyekuwa dereva wake Sh790,398 aliyefutwa kazi kwa kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mfanyakazi mwenza.
Dominic Mutuku Mulavu, aliyefanya kazi ya udereva katika shirika la World Vision kwa miaka 12, alipigwa kalamu Mei 2024 kwa madai ya kukiuka Sera ya Ulinzi ya shirika hilo.
Mwajiri wake alidai kuwa Bw Mutuku alijihusisha na uhusiano uliopigwa marufuku na mwanamke huyo kinyume cha sera ya kampuni.
Ajira yake ilifutwa kuhusiana na madai kwamba alijihusisha na uhusiano uliopigwa mwanamke huyo, mwanajamii katika eneo la Mutumo, Kaunti ya Kitui.
Hata hivyo, ushahidi uliowasilishwa mbele ya Mahakama ya Leba na Mahusiano ya Ajira ulionyesha mwanamke huyo ni mfanyabiashara huru, wala si anayenufaika, na kwamba uhusiano wao wa miaka mitatu ulikuwa wa hiari na ulinuiwa kufunga ndoa.
Mwajiri alishindwa kuthibitisha vinginevyo.
Korti ilibaini kwamba hatua ya kufuta kazi haikuwa ya haki.
Ingawa korti ilisema mchakato wa nidhamu ulifuata viwango vilivyowekwa, mwajiri alitumia visivyo sera yake binafsi katika uhusiano halali wa kibinafsi.
Kwa kuzingatia haya yote, korti haijaridhishwa kwamba mshtakiwa (World Vision) amethibitisha sababu ya kufuta ajira ya mlalamishi (Mulavu) ilikuwa halali, ya haki na yenye mantiki kuambatana na maana ya Sheria kuhusu Ajira,” alisema Jaji Stella Rutto.
“Baada ya kubaini sababu iliyotolewa kumfuta kazi mlalamishi haikuwa ya haki, halali na yenye mantiki, korti imeamuru mlalamishi alipwe mshahara wa mwezi mmoja kabla ya notisi kiasi cha Sh87,822.00, pamoja na fidia ya Sh702,576.00, sawa na mshahara wa miezi minane kabla ya kukatwa ushuru.”
Fidia hii inaashiria karibu muda wa miaka 12 wa uhusiano wa ajira na ushahidi kuwa taaluma ya mlalamishi ilikatizwa kabla ya wakati.