Habari za Kitaifa

Vyuo 10 haviwezi kueleza vilivyotumia Sh3 bilioni

Na ERIC MATARA February 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

UBADHIRIFU wa Fedha unaoendelea kwenye vyuo vikuu umeanikwa ambapo vyuo 10 vilitumia Sh3 bilioni bila stakabadhi zozote za kuonyesha jinsi ambavyo pesa hizo zilitumika.

Mkaguzi wa Hesabu za Serikali Nancy Gathungu amelalamika kuwa ufisadi umepiga kambi vyuo vikuu kiasi kwamba Sh2.8 bilioni zilifujwa.

Vyuo vikuu hivyo 10 ni Kenyatta, Moi, Nairobi, Kabianga, Egerton, Jaramogi Oginga Odinga, Murangá, Maasai Mara, TUK na TUM.

Chuo Kikuu cha Egerton kinachopatikana Kaunti ya Nakuru kilitumia Sh6.3 milioni kuwalipa malandilodi wawili ambao hawana mkataba na chuo hicho.

Kile cha Murang’a nacho kilitumia Sh786,060 kama marupurupu kwa usafiri wa ndege na barabarani kwa wanachama wa baraza la chuo hicho.

Ubadhirifu huo ulianikwa pia katika Chuo Kikuu cha Nairobi ambapo Sh1.78 bilioni zilitumika kulipia malazi na chakula pamoja na vibarua ilhali hakuna stakabadhi za kuunga matumizi hayo.

“Chuo hakikutoa stakabadhi za kuunga matumizi ya Sh133.9 milioni, Sh662, 662 zilizotumika na baraza la chuo na Sh1.64 bilioni kuwalipa vibarua,” ikasema ripoti ya Bi Gathangu ya mwaka wa kifedha uliokamilika mnamo 2024.

Ndani ya kipindi hicho, Kabianga nacho kililipa Sh22.5 milioni kwa Kampuni ya Telkom kwa kukodisha ardhi yao ilhali hakukuwa na ushahidi wa muafaka kati yao.