Michezo

Kiini cha kifo cha mchezaji wa KK Homeboyz sasa chabainika

Na WYCLIFFE NYABERI February 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

ALIYEKUWA mchezaji wa Kakamega Homeboyz, Sailas Abung’ana alifariki kutokana na damu kuganda katika ubongo wake.

Hali hiyo ilisababishwa na kugongwa kichwani na kifaa butu.

Hii ni kulingana na ripoti ya upasuaji uliofanyiwa maiti yake Jumatatu katika Hospitali Kuu ya Kaunti ya Kakamega.

Abung’ana alifariki wiki mbili zilizopita baada ya kuzozana na kakake mdogo, Denmark Muchiti.

Muchiti ndiye anayedaiwa kumpiga Abung’ana kwa kifaa hicho nyumbani kwao kijijini Muranda, eneobunge la Shinyalu, Kakamega.

Kutokana na shutuma hizo, Muchiti alikamatwa na kufikishwa kortini japo hajasomewa mashtaka kwa kuwa wapelelezi waliomba muda wa wiki mbili kukamilisha uchunguzi wao, unaohusisha kumfanyia mshukiwa vipimo vya kiakili.

Anatarajiwa kurudishwa mahakamani Februari 23.

Hayo yakijiri, mipango ya mazishi ya Abung’ana inakaribia kufika tamati kwani kamati andalizi imeteua siku ya kumzika mchezaji huyo.

Abung’ana atazikwa Jumamosi, Februari 21 nyumbani kwa wazazi wake kijijini Muranda, kwenye eneobunge la Shinyalu.

Mwili wa mwendazake unatarajiwa kuondolewa katika makavani ya hospitali kuu ya Kakamega siku ya Ijumaa, ambapo utapelekwa katika uwanja wa Bukhungu ili kutoa nafasi kwa wachezaji na mashabiki wa Homeboyz kuutazama.

Baadaye, utasafirishwa hadi kijijini Muranda siku hiyo ya Ijumaa kabla ya mazishi yake Jumamosi.

Abung’ana alijiunga na Homeboyz mwanzoni mwa msimu huu kutoka klabu ya Supaligi (NSL) ya Gucha Stars FC yenye maskani yake Sameta, Kaunti ya Kisii.

Abung’ana pia alikuwa katika kikosi kilichoisaidia Shabana FC kupandishwa daraja hadi Ligi Kuu mwaka wa 2023 kutokea NSL.

Alikuwa kiungo muhimu kwa kikosi cha kocha Sammy Okoth kilichopandisha Shabana daraja hadi Ligi Kuu baada ya miaka 17.

Wawili hao baadaye waliondoka Glamour Boys na kuungana tena kambini Gucha Stars FC, ambayo wakati huo ilikuwa ikishiriki Divisheni ya Kwanza.

Msimu mmoja baada ya kujiunga na Gucha, wawili hao waliisaidia timu hiyo kupanda daraja hadi NSL ambako inacheza kwa sasa.