Mpango wa kujenga ukuta mpaka wa Somalia ulivyokosa kutekelezwa licha ya kumeza Sh3.4b
UAMUZI wa Kenya kujenga ukuta wa usalama mpakani mwa Somalia haukuwa kazi rahisi kamwe.
Lengo lilikuwa kuzuia magaidi wa Al-Shabaab waliokuwa wakitekeleza mashambulizi ya kikatili katika eneo la Kaskazini Mashariki, Pwani na hata jijini Nairobi.
Mradi huo uliozinduliwa mwaka 2015 ulikuwa wa kujenga kizuizi cha kudumu katika mpaka wa takriban kilomita 700 kutoka Mandera hadi Bahari ya Hindi kwa gharama iliyokadiriwa kuwa Sh8 bilioni.
Utekelezaji uliwekwa chini ya Wizara ya Ulinzi badala ya Usalama wa Ndani iliyoubuni.
Hata hivyo, mpango wa awali wa kujenga ukuta mkubwa ulibadilika na kuwa ua wa waya, jambo lililozua maswali mengi.
Kufikia mwaka 2019, Bunge la Kitaifa lilielezwa kuwa ni kilomita 10 pekee zilikuwa zimejengwa kwa gharama ya Sh3.4 bilioni, kiwango ambacho kingesababisha matumizi ya zaidi ya Sh200 bilioni kukamilisha mradi huo.
Mradi ulipangwa kutekelezwa katika sehemu tatu: sekta ya kaskazini kutoka Mandera hadi Elwak, ya kati kutoka Elwak hadi Libat, na ya kusini kutoka Libat hadi Kiunga.

Ukuta huo ulipangwa kuwa na vituo vya usalama, kamera za ufuatiliaji na vizuizi vya kudhibiti uhamiaji haramu.
Lakini hali halisi mpakani ni tofauti. Leo, kuna mwingiliano huru wa watu, magari, pikipiki na mikokoteni kati ya Mandera na Bula Hawa nchini Somalia.
Njia rasmi ya forodha imesalia bila shughuli huku njia zisizo rasmi zikishamiri.
Baadhi ya wakazi wanasema hakuna mpaka uliofungwa kwa vitendo. Wengi huvuka asubuhi kuingia Kenya na kurejea Somalia jioni bila kuulizwa kibali cha kusafiria.
Biashara pia hufanyika bila ukaguzi wa ubora wa bidhaa.
Wakati huo huo, mjadala mkali uliibuka bungeni mwaka 2019 kuhusu ufanisi wa ua wa waya.
Wabunge walipinga mgao zaidi wa fedha na kuitaka serikali iwajibike kwa mabilioni yaliyotumika. Mradi huo baadaye ulikabidhiwa Wizara ya Usalama wa Ndani.
Ziara katika eneo hilo inaonyesha nguzo za simiti zilizovunjwa, ishara ya uharibifu.
Mradi pia ulikumbwa na changamoto za ufadhili, malipo ya wafanyakazi wa Huduma ya Vijana kwa Taifa na hata mvutano wa kidiplomasia kati ya Kenya na Somalia.
Wiki iliyopita, Rais William Ruto alitangaza mjini Mandera kuwa mpaka huo utafunguliwa rasmi mwezi Aprili, karibu miaka 15 tangu kufungwa.
Alisema hatua hiyo imechukuliwa baada ya tathmini za kina za usalama na kuahidi kuimarisha ulinzi.
Hata hivyo, taasisi ya uchambuzi wa masuala ya usalama ya Hiraal Institute imeonya kuwa Al-Shabaab inaendelea kuimarika.
Swali kuu linasalia: Je, kufunguliwa kwa mpaka kutaleta nafuu ya kiuchumi bila kuhatarisha usalama wa taifa?