Msaidizi wa Jumwa ataka arudishiwe bastola yake baada ya kesi ya mauaji kusambaratika
ALIYEKUWA msaidizi wa Aisha Jumwa, Geoffrey Okuto, amerejea mahakamani akiomba arudishiwe bastola yake iliyochukuliwa na polisi baada ya kukamatwa kwake kwa tuhuma za kumuua mfuasi wa chama cha ODM miaka sita iliyopita.
Katika hati zake za mahakama, Bw Okuto anasema kesi hiyo ilikamilika na akaachiliwa huru baada ya mahakama kubaini kuwa hakuwa na hatia.
“Bastola ilikuwa yangu na nilikuwa na leseni halali. Ningependa kurudishiwa silaha hiyo kwa kuwa niliimiliki kisheria baada ya kusajiliwa kama mmiliki wa bunduki,” alisema.
Hata hivyo, upande wa mashtaka umeomba muda wa kushauriana na idara ya polisi kabla ya silaha hiyo kurejeshwa kwake.
Mahakama pia imeamuru arejeshewe paspoti yake ambayo imekuwa ikihifadhiwa mahakamani tangu alipokamatwa.
Bw Okuto aliambia mahakama kuwa anahitaji paspoti hiyo kwa safari za kibiashara nje ya nchi.
“Nina safari ya kwenda nje ya nchi na paspoti yangu bado iko mahakamani. Naomba irejeshwe kwa kuwa kesi yangu ya mauaji ilikamilika,” alisema.
Polisi walichukua bastola na paspoti hiyo wakati Bw Okuto alipokuwa akikabiliwa na kesi ya mauaji ya Jola Ngumbao.
Serikali ilimshtaki kwa kumuua Ngumbao mnamo Oktoba 15, 2019, wakati wa mzozo uliotokea katika wadi ya Ganda, Kaunti ya Kilifi.
Upande wa mashtaka ulidai kuwa Bw Okuto alimpiga risasi Ngumbao.
Hata hivyo, baada ya kusikiliza ushahidi kutoka kwa mashahidi 12, mahakama ilimuachilia huru ikisema mashtaka hayakuthibitishwa.
Mahakama ilieleza kuwa upande wa mashtaka haukuwasilisha ushahidi wa kutosha kuthibitisha kuwa Bw Okuto ndiye aliyefyatua risasi iliyomuua Ngumbao.
“Upande wa mashtaka umeshindwa kuthibitisha kesi ya mauaji dhidi ya mshtakiwa bila shaka yoyote. Kwa hivyo, mshtakiwa anaachiliwa huru kwa kosa la mauaji,” mahakama ilisema mwaka jana.
Mahakama iliongeza kuwa ushahidi uliotolewa haukumhusisha moja kwa moja na kifo cha Ngumbao.
Kati ya mashahidi 12, ni mmoja tu aliyedai kumuona Bw Okuto akifyatua risasi katika boma la mjomba wa marehemu, Bw Reuben Katana, ambako kulikuwa na mafunzo ya maafisa wa uchaguzi mdogo wa ODM.
Hata hivyo, mahakama ilitupilia mbali ushahidi huo kwa kukosa uaminifu kutokana na kauli zinazokinzana.
Shahidi huyo alidai alimuona Bw Okuto akifyatua risasi mara mbili, lakini katika maelezo mengine alisema alipiga risasi mara tatu.
Hapo awali, Bw Okuto alishtakiwa pamoja na Bi Jumwa, lakini baadaye aliondolewa shtaka baada ya Rais William Ruto kumteua kuwa Waziri wa Jinsia kufuatia Uchaguzi Mkuu wa 2022.
Upande wa mashtaka uliiambia mahakama kuwa baada ya kupitia ushahidi, ilibainika kuwa Bi Jumwa hakuhusishwa na mauaji ya Bw Ngumbao.