Makala

Mshtakiwa mwenza wa Obado katika kesi ya mauaji ya Sharon akosa kufika kortini

Na RICHARD MUNGUTI February 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MAHAKAMA kuu imemwagiza Michael Oyamo anayeshtakiwa pamoja na Gavana wa zamani Migori Okoth Obado kwa mauaji ya mwanafunzi wa chuo kikuu cha Rongo Sharon Otieno miaka saba iliyopita hakufika kortini wakati wa mawasilisho ya mwisho.

Jaji Cecilia Githua alielezwa na wakili wa Oyamo kwamba “msaidizi huyo wa zamani wa Obado ni mgonjwa na amelazwa hospitali.”

Kiongozi wa mashtaka Bi Gikui Gichuhi alieleza mahakama hakuna stakabadhi za hospitali kuthibitisha Oyamo ni mgonjwa na amelazwa.

Washtakiwa hao Obado, Oyamo na Caspal Obiero walikuwa wameamriwa wafike kortini kuwasilisha tetezi zao za mwisho kabla ya adhabu kutolewa ikiwa walihusika na mauaji ya Sharon au la.

Kufuatia kutofika kwa Oyamo mahakamani ilibidi Jaji Githua asitishe kesi hiyo hadi Machi 18,2026.

Mahakama ilimwamuru Oyamo awasilishe ushahidi kutoka hospitali kuthibitisha alikuwa mgonjwa.

Watatu hawa wamekana walimuua Sharon na mtoto wake katika msitu ulioko kaunti ya Migori mnamo 2019.

Ushahidi wa uchunguzi wa DNA uliowasilishwa kortini ulithibitisha kwamba Obado ndiye alikuwa baba ya mtoto aliyeuawa pamoja na Sharon.

Upande wa mashtaka umeomba mahakama kuu iwapate na hatia Obado , Oyamo na Obiero ya kumuua Sharon.

Lakini Obado ameomba aachiliwe akisema alikuwa anamsaidia Sharon na alikuwa amepanga kumnunulia shamba na kumjengea nyumba ya kuishi yeye na mwanaye.

Kesi hiyo itatajwa Machi 18,2026 kutengewa siku ya hukumu.